Na Mwandishi Wetu
BALOZI wa Tanzania nchini Comoro, Saidi Yakubu leo amekutana na wachezaji wa zamani wa timu ya Taifa ya Comoro ambao wameipongeza timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kwa mafanikio waliyoyapafa kwenye michuano ya kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2025) inayoendelea nchini Morocco.
Wachezaji hao Hamdani Raffiou na Adinane Ismael ambayo wameichezea timu ya Comoro kwa nyakati tofauti wameelezea kufurahishwa na matokeo waliyoyaona na historia iliyowekwa na Taifa Stars kwa kufika hatua ya 16 bora kwa mara ya kwanza katika historia ya ushiriki wa Tanzania kwenye AFCON.
“Tumeona ubora wa soka la Tanzania kwa sasa umepanda sana na tunawapongeza kwa mafanikio kwenye soka la Afrika” amesema Bwana Hamdani Raffiou aliyeongoza wenzake kutembelea ubalozi wa Tanzania.

Aidha wachezaji hao ambao kwa sasa wanachezea timu ya Ntsaoueni Veterans ambao ndio mabingwa wa michuano ya maveterani nchini Comoro waliwasilisha pia azma ya timu yao kutembelea Tanzania mwezi Machi,2026.
Kwa upande wake Balozi Saidi Yakubu aliwashukuru kwa pongezi hizo na kuwaelezs kuwa mafanikio ya Taifa Stars ni matokeo ya uwekezaji wa Serikali kwenye uendelezaji wa vipaji,uendelezaji wa miundombinu ya michezo,uongozi mahiri wa sekta ya michezo na mapenzi ya dhati ya mashabiki wa soka kwa timu yao ya Taifa.


