Na Winfrida Mtoi
Kocha Mkuu wa timu ya Pamba Jiji, Francis Baraza amesema hana presha yoyote kuelekea mchezo wao wa kesho dhidi ya Yanga kutokana na alivyojipanga, akijivunia mbinu zake.
Amesema anaamini ana wachezaji wazuri wanaoweza kutoa ushindani kwa Yanga, hivyo ataingia uwanjani kuonesha burudani ya soka kwa kushambulia na si kwenda kuzuia ‘kupaki basi’ kama wengi wanavyotarajia.
“Mifumo yote mimi nitaipiga, mshakuwa na ile kuwa tutapoteza lakini dakika 90 zitaongea. Najua Yanga ni mabingwa, ni timu imechukua mara nne. Ila mimi sina presha, nikiweka presha nitawaumiza wachezaji wangu,” amesema Baraza.

Kocha huyo raia wa Kenya, amesema kwa kawaida anapokutana na timu kubwa huwa anatumia nafasi hiyo kuwapa fursa wachezaji wake hasa wadogo ili kuonesha uwezo wao na kuthibisha hilo kesho atamuanzisha kijana wa umri chini ya miaka 20 (U -20).
Ameeleza kuwa pamoja na kuwa nchini Kenya lakini anafuatilia Ligi ya Tanzania, msimu mzima uliopita ameifuatilia mechi za Pamba na anajua ni sehemu gani ina shida anaendelea kurekebisha.
Yanga na Pamba zitakutana katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam, ikiwa ni mechi ya kwanza ya msimu mpya kwa Yanga ambayo ni bingwa mtetezi na mchezo wa pili wa Pamba.