Na Mwandishi Wetu
Wafanyabiashara ya miwani nchini wametakiwa kizingatia sheria na kuacha kuuza kuholela ikiwamo kuchanganya na bidhaa nyingine kwani miwani ni tiba, hivyo inaweza kumuathiri mtumiaji.
Hayo yamebainishwa na Msajili wa Baraza la Optometria nchini, Sebastiano Millanzi wakati wa kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya miwani, Agosti 18, 2025 katika Soko la Kabwe lililopo jijini Mbeya.
Wakati wa utoaji elimu hiyo,imebainika kuwepo kwa baadhi ya wafanyabishara ambao hawana taaluma ya Optometria lakini wanajihusisha na uuzaji wa miwani bila kuwapima watu, huku wakiiuza pamoja na bidhaa nyingine mbalimbali za urembo kinyume na miongozo iliyopo.
Milanzi amesema ni vema anayetaka kujihusisha na biashara ya miwani azingatie sheria Optometria sura namba 23 ikiwemo kusajiliwa katika Baraza hilo.

“Kutokujua sheria sio sababu ya kuvunja sheria na ni bahati kuwa ninyi mlikuwa bado hamjapata elimu hii, hivyo kwa sasa tunawapa elimu pamoja na kuwataka kusitisha hadi pale mtakapokamilisha taratibu stahiki za usajili kuanzia ngazi ya Mganga Mkuu wa Jiji, amesisitiza Millanzi.
Aidha ametumia wasaa huo kuziagiza mamlaka za usimamizi ngazi ya halmashauri na mkoa kuwa na muendelezo wa usimamizi shirikishi wa mara kwa mara na kutoa elimu endelevu kwa wananchi.
Kwa upande wao wafanyabiashara hao wamekiri kufanya biashara hiyo bila kujua kuwa wanakiuka taratibu, hivyo wakaahidi kuzingatia maagizo yaliyotolewa kwao ya kuanza taraibu za usajili.