Na Winfrida Mtoi
Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, imeahidiwa kiasi cha fedha shilingi bilioni moja kama zawadi, ikifanikiwa kutwaa ubingwa wa michuano ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN 2024) inayotarajiwa kuanza Agosti 2 – 28, 2025.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi, amesema ahadi hiyo imetolewa na Rais Samia Suluhu Hassan, ikiwa ni motisha, wakiamini timu hiyo itapambana kupeperusha vyema bendera ya nchi.

“Naomba niwatangazie umma wa watanzania kuwa, katika kuchagiza hamasa kwa timu yetu ya Taifa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan ametoa ahadi ya donge nono la fedha za Kitanzania shilingi bilioni moja kwa vijana wetu wa Taifa Stars iwapo watafanikiwa kutwaa ubingwa wa mashindano haya ya CHAN 2024,” amesema Prof. Kabudi.
Aidha amewataka watazanzania kujitokeza kwa wingi katika mechi za mashindano hayo, hasa siku ya mechi ya ufunguzi ambapo Tanzania itacheza na Burkina Faso Agosti 2, 2025, Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Gerson Msigwa, amefafanua kuwa mtindo wa goli la mama unaendelea ambapo Rais Samia atanunua kila goli moja la ushindi kwa Taifa Stars kwenye kila mechi ya makundi na robo fainali kwa sh 10 milioni na endapo itafika hatua ya nusu fainali atanunua kila goli kwa sh 20 milioni.
Katika michuano hiyo, Taifa Stars ipo kundi B, ikiwa na timu za Burkina Faso, Mauritania, Jamhuri ya Afrika ya Kati na Madagascar ambazo zitatumia Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam.