Na Tatu Mohamed
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinzudi, Dkt. Hussein Ally Mwinyi, anatarajiwa kufungua maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam 2025, Julai 7, mwaka huu.
Maonesho hayo ambayo yalianza Juni 28, mwaka huu yatafungwa Julai 13, mwaka huu na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Akizungumza jijini Dar es Salaam baada ya kutembelea Maonesho hayo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt Selemani Jafo alisema katika maonesho hayo yanaongozwa na kaulimbiu ‘Maonesho ya Biashara ya Kimataifa fahari ya Tanzania’ kutakuwa na washiriki 3887 kutoka nchi 23 na makampuni 386 ya kimataifa.

Aliwataka Watanzania kushiriki kwa ukubwa maonesho hayo ambayo ni makubwa zaidi kutokana na ushiriki wa mataifa mbalimbali.
“Hii ni fursa ya Watanzania kujitangaza kimataifa kutokana na kuwepo na wafanyabiashara wakaubwa Afrika, pia kutakuwa na uzinduzi wa nembo yetu ambapo tunamtarajia Naibu Waziri Mkuu, Dk. Doto Biteko, kuizindua,” alisema.
Alisema kulikuwa na makampuni zaidi ya 90 ambayo yanashindanishwa, kwa sasa yamebaki matatu na atatakiwa kubaki mmoja ambaye atatangazwa siku ya uzinduzi.

Dk. Jafo aliwaomba Watanzania kushirikiana kwa pamoja katika jambo hilo kubwa ambalo litaacha alama kubwa hapa nchini.
Alisisitiza kuwa serikali imejipanga vyema katika viwanda na biashara hivyo watahakikisha maonesho hayo yanachangia katika ukuaji wa uchumi wa taifata.
Pia, aliwasisitiza Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki uchaguzi mkuu wa serikali Oktoba, mwaka huu lakini kubwa kudumisha amani ya nchi.