Na Mwandishi Wetu
WAKATI Dunia ikiadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika wito umetolewa kwa wazazi na walezi kuwafunza watoto maadili ili kuwa na jamii bora.
Wito huo umetolewa na Mganga Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Dkt. Jonas Lulandala wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika katika Shule ya Longquan wilayani Temeke.
Maadhimisho hayo yameandaliwa na Taasisi ya Mabudha inayomiliki Shule ya Longquan na kushirikisha vituo 13 vya kulelea watoto yatima ambavyo pia vimepatiwa misaada mbalimbali ya kibinadamu.

“Ni jukumu letu kuwafundisha watoto maadili, kuwafundisha kumtambua Mwenyezi Mungu kwa sababu huo ndio msingi mkubwa wa malezi. Mtoto ambaye hataweza kumtambua Mwenyezi Mungu maana yake hawezi kuwa na hofu ya Mungu tutakuwa na jamii yenye amani, upendo na inayoweza kuishi vizuri, ” amesema Dkt. Lulandala.
Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Awali na Msingi ya Longquan, Jane Shao, amesema shule hiyo pia inamiliki kituo cha kulelea watoto ambapo wamekuwa wakiwasomesha bure wale wanaotoka kwenye mazingira magumu.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shule ya Longquan, Master Xian Hong, amesema kila mwaka wamekuwa wakialika watoto na walezi kutoka katika vituo mbalimbali kusherehekea pamoja Siku ya Mtoto wa Afrika pamoja na kuwapa mahitaji mbalimbali.

Kaulimbiu ya maadhimisho mwaka huu inasema Haki za Mtoto: Tulipotoka, Tulipo na Tuendako ‘Maendeleo Endelevu 2030: Imarisha Ulinzi na Fursa Sawa kwa Watoto.
