Na Mwandishi Wetu
Chama Cha Kuogelea Tanzania (TSA), kimehitimisha msimu wa mashindano kwa mujibu wa kalenda yao kwa kupata mabingwa katika michuano ya Taifa ya watoto wenye umri kuanzia miaka 5-12 yaliyomalizika jana Juni 15, 2025, jijini Dar es Salaam.
Katika mashindano hayo yaliyoshirikisha klabu 18, moja ikiwa imealikwa kutoka Mombasa, Kenya, jumla ya wachezaji 295 walioshiriki walishindana katika mitindo tofauti tofauti na washindi kutunukiwa medali na vikombe.

Akizungumza wakati wa kufunga mashindano hayo, Ofisa Michezo Mwandamizi wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Charles Maguzu, ameupongeza uongozi wa TSA na kuvitaka vyama vingine vya michezo hapa nchini kuwa na utaratibu wa kualika timu za nchini jirani katika mashindano yao.

Amesema amefurahia kuona klabu kutoka Kenya imealikwa kushiriki mashindano hayo, kwani kufanya hivyo ni kuzidi kuendeleza vipaji pamoja na kuimarisha umoja wa nchi hasa za Afrika Mashariki kukuza mahusiano ya Kimataifa kupitia diplomasia ya michezo.
“Kwa namna ya kipekee napenda kupongeza chama cha mchezo wa kuogelea kwa kuweza kuandaa mashindano makubwa kama haya na idadi ya washiriki inazidi kuongezeka siku hadi siku,, hii inaonyesha ni jinsi gani chama kimejipanga.
“Niwapongeze pia kwa kuweza kualika klabu kutoka Mombasa Kenya. Vyama vingine vya michezo vinatakiwa kufanya kama hivi, vinapoandaa mashindano vijitahidi kushirikisha timu za nchi jirani ili kukuza uhusiano wa kidiplomasia,” ameeleza.

Aidha ameutaka uongozi wa TSA usisite kwenda BMT kuomba msaada pale unapokwama ili kushirikiana kuendeleza mchezo huo na kufikia malengo waliyojiwekeza.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa TSA David Mwasyoge, amesema mashindano hayo yamekwenda vizuri, vipaji vimeonekana hivyo anaamini watakuwa na waongeleaji bora katika michuano ya kimataifa.
“Tunaomba wadau waendelee kutusapoti, mchezo wa kuogelea ni mchezo unaotumia gharama kubwa. Watusaidie kifedha, kiushauri ili tuweze kuendeleza huu mchezo na kufika mikoa mingi zaidi,” amesema.