📍Kigamboni, Dar es salaam
📌Wananchi kuunganishiwa huduma kwa mkopo
Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA)imefanya kazi kubwa ya kuhakikisha wananchi wa Kigamboni wanapata huduma ya uhakika ya majisafi na salama, kwa kutekeleza miradi mikubwa ya miundombinu ya maji.
Akizungumza wakati wa ziara ya Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025 leo Juni 2, 2025 Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), Mhandisi Mkama Bwire, amesema moja ya mafanikio makubwa ni ujenzi wa tanki kubwa la kuhifadhi maji lenye ujazo wa lita milioni 15, ambalo tayari limekamilika.

“DAWASA inatoa huduma ya kuunganishia maji kwa wananchi wote wanaohitaji, na kwa wale ambao hawana uwezo wa kulipia mara moja, wanaweza kuunganishwa kwa mkopo, wafike katika ofisi zetu na kufata taratibu lengo kubwa ni kuongeza kasi ya wananchi wengi kuingia katika mtandao wa maji” amesema Mhandisi Bwire.
Akikagua mradi huo Kiongozi wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi ameupitisha mradi wa maji wa Kigogo na kuipongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kwa utekelezaji wa matumizi ya mita za Malipo ya Mita ya malipo ya Kabla (Pre-paid meters) huduma ambayo italeta mapinduzi katika utoaji huduma.
Aidha, Ussi ametoa pongezi hizo, wakati Mwenge wa Uhuru ulipotembelea na kukagua mradi wa usambazaji maji mtaa wa Kigogo, katika Kata ya Kisarawe II ambapo mradi unatekelezwa na DAWASA.

“Jitihada hizi DAWASA mnazoendelea kuzionyesha za kufunga mfumo huu unaleta tija kubwa kwa wananchi kwa kuwa inarahisisha upatikanaji wa huduma na kuwezesha kutimiza adhima ya Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi mahiri wa Rais wetu Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan katika utoaji wa huduma nzuri kwa wananchi wake kwa hilo niwapongeze tuendelee kufanya kazi nzuri kwa maslahi mapana ya nchi yetu” amesema Ussi.
Amesema Mwenge wa Uhuru Kitaifa umepitia taarifa na kukagua mradi umeridhika na utekelezaji wa mradi uliotekelezwa kwa Gharama ya Shilingi Milioni 780 kwa lengo la kuhudumia wananchi 6,729 wa Mtaa wa Kigogo katika Kata ya Kisarawe II.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Halima Bulembo amesema kuwa ujio wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa umeleta unafuu kwa wananchi wa Kata ya Kisarawe II mtaa wa Kigogo ambao wamekuwa kwenye changamoto ya maji kwa muda mrefu.