Na Tatu Mohamed
TANZANIA inaandika ukurasa mpya katika historia ya sekta ya nishati leo Agosti 22, 2026, wakati Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan akizindua rasmi Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), mradi mkubwa wa kimkakati unaotarajiwa kuongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.
Uzinduzi huo unafanyika baada ya kukamilika kwa mitambo yote tisa ya mradi huo yenye uwezo wa kuzalisha jumla ya Megawati 2,115, hatua inayotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa matumizi ya wananchi, shughuli za uzalishaji na uwekezaji.
Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere umegharimu takribani Shilingi trilioni 7.452, huku ukifadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati inayolenga kuimarisha uchumi wa taifa.
Kukamilika kwa mradi huo kunatajwa kuwa hatua muhimu katika safari ya Tanzania ya kuongeza uzalishaji wa umeme na kuweka mazingira bora kwa maendeleo ya viwanda, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi zinazohitaji nishati ya uhakika.
Bwawa hilo pia lina umuhimu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kuifanya nishati kuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi, maendeleo ya viwanda, uwekezaji, ubunifu na ustawi wa wananchi, huku uzinduzi wa leo ukiwa kilele cha safari ya utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kitaifa.


