Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WAKALA wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) umesema mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja umeifanya Tanzania kuendelea kuwa kitovu muhimu cha usambazaji wa mafuta kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, hatua inayochochea biashara ya kikanda na kuongeza mchango wa sekta ya nishati katika uchumi wa taifa.
Akizungumza katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima ‘Nanenane’ yanayoendelea jijini Dodoma, Mhandisi wa Petroli wa PBPA, Rehema Mahundi, amesema mbali na kuhakikisha mafuta yanapatikana kwa uhakika nchini, wakala huo umewezesha pia nchi jirani kunufaika na miundombinu ya bandari za Tanzania.

“Kupitia mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja, Tanzania siyo tu inahudumia mahitaji yake ya ndani, bali pia inatoa huduma kwa nchi jirani kama Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Uganda, Malawi na Zambia. Hii inaifanya nchi kuwa kitovu muhimu cha biashara ya mafuta katika ukanda wetu,” amesema Mahundi.
Amesema PBPA husimamia mchakato mzima wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja kupitia zabuni za kimataifa zinazofanyika kila mwezi, ambapo mikataba huandaliwa kwa kuzingatia mahitaji ya mafuta ya miezi miwili ijayo.Kwa mujibu wa Mahundi, utaratibu huo umeondoa changamoto za upatikanaji wa mafuta na kuifanya Serikali kuwa na uwezo wa kupanga mahitaji ya nchi kwa ufanisi zaidi.

“Tunapanga uagizaji mapema kulingana na mahitaji halisi ya soko. Hii inahakikisha mafuta yanapatikana wakati wote na shughuli za uzalishaji, usafirishaji na biashara haziathiriki,” amesema.
Ameeleza kuwa mfumo huo umeongeza uwazi katika sekta ya mafuta kwa kuwezesha Serikali kuwa na takwimu sahihi za mafuta yaliyopo nchini, yanayoingia na yanayotarajiwa kuwasili, jambo linalorahisisha usimamizi wa sekta hiyo.
Amesema upatikanaji wa mafuta kwa uhakika ni nguzo muhimu ya maendeleo ya sekta mbalimbali za uchumi, zikiwemo viwanda, kilimo, usafirishaji na utalii, ambazo zinategemea nishati hiyo kuendesha shughuli zake.

Ameongeza kuwa PBPA itaendelea kuboresha mfumo wa uagizaji wa mafuta ili kuhakikisha Tanzania inabaki kuwa lango la uhakika la usambazaji wa mafuta katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, sambamba na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Aidha, amewataka wananchi kutembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Nanenane ili kupata elimu kuhusu majukumu ya wakala huo na namna mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja unavyochangia maendeleo ya uchumi wa Tanzania na nchi jirani.


