Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC) limesema ushirikiano wake na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) umechangia kuongeza uzalishaji wa karafuu visiwani Zanzibar kupitia mikopo nafuu inayowawezesha wakulima kuboresha shughuli za kilimo.
Akizungumza katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima ‘Nanenane’ yanayoendelea jijini Dodoma, Afisa Masoko wa ZSTC, Majid Najim amesema benki hiyo imekuwa mshirika muhimu kwa kutoa mikopo inayowafikia wakulima pamoja na kuwawezesha kupata huduma mbalimbali za kuongeza tija katika uzalishaji.
“Kupitia mikopo ya TADB tumekuwa tukiwasaidia wakulima kupata nyenzo muhimu za uzalishaji wa karafuu, ikiwemo kuchimbiwa visima, kuanzishiwa vitalu na kupatiwa miche bila malipo. Hii imechangia kuongeza uzalishaji wa zao hili muhimu la biashara,” amesema.

Amesema ZSTC ni miongoni mwa wazalishaji wakuu wa karafuu nchini, huku pia ikizalisha mafuta muhimu (essential oils) na viungo (spices) vinavyolimwa kwa mfumo wa kilimo hai kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi.
Ameeleza kuwa pamoja na kuwezesha uzalishaji, TADB imekuwa ikitoa elimu ya usimamizi wa fedha kwa wakulima ili kuhakikisha mapato wanayopata baada ya mavuno yanatumika kuendeleza shughuli za kilimo na kuboresha maisha yao.
“Kilimo hakiishii shambani. Baada ya mavuno, mkulima anatakiwa kujua namna bora ya kutumia kipato chake ili aweze kuwekeza tena na kuongeza uzalishaji. TADB imekuwa ikishirikiana nasi kutoa elimu hiyo ya fedha kwa wakulima wetu,” amesema.
Ameongeza kuwa ushirikiano huo umeiwezesha Zanzibar kuongeza jitihada za kuendeleza kilimo cha karafuu, hususan katika kisiwa cha Pemba, ambako zao hilo linaendelea kuwa chanzo kikuu cha mapato kwa wakulima wengi.
Amewataka wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nanenane kufika katika banda la ZSTC ili kujifunza kuhusu bidhaa mbalimbali zinazotokana na karafuu na viungo vya Zanzibar pamoja na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa zao hilo.


