Na Tatu Mohamed
MAMLAKA ya Serikali Mtandao (e-GA) imeeleza kuwa inaendelea kushirikiana na Wizara ya Kilimo kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali inayorahisisha utoaji wa huduma, kuongeza uwazi na kuboresha usimamizi wa shughuli mbalimbali za kilimo nchini.
Akizungumza katika Maonesho ya kitaifa ya wakulima ‘Nanenane’ yanayoendelea jijini Dodoma, Meneja Mawasiliano wa e-GA, Subira Kaswaga, amesema mamlaka hiyo imekuwa ikibuni na kusimamia mifumo ya TEHAMA inayosaidia taasisi mbalimbali kuboresha utendaji kazi na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.
Amesema miongoni mwa mifumo iliyotekelezwa ni ule unaoiwezesha Wizara ya Kilimo kupata taarifa za wakulima, kufuatilia shughuli za taasisi zilizo chini ya wizara hiyo pamoja na kutoa taarifa muhimu za kilimo kwa wadau.

Ameongeza kuwa e-GA pia imeshirikiana na Tume ya Maendeleo ya Ushirika kutengeneza mfumo wa usimamizi wa vyama vya ushirika, unaowawezesha wakulima kufuatilia mauzo ya mazao yao, bei pamoja na malipo wanayostahili kupokea, huku ukiongeza uwazi na uwajibikaji katika uendeshaji wa vyama hivyo.
“Mpaka sasa zaidi ya vyama 6,000 vya ushirika vinatumia mfumo huo, ambao umechangia kuboresha usimamizi wa mapato na kuimarisha uwajibikaji katika sekta ya ushirika,” amesema.
Aidha, amesema e-GA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) imeanzisha Fertilizer Information System (FIS), unaowezesha kusimamia wazalishaji na waingizaji wa mbolea, kufuatilia mwenendo wa soko pamoja na kuhakikisha wauzaji wanazingatia bei elekezi.
Amesema mfumo huo umeimarisha usimamizi wa soko la mbolea na kusaidia upatikanaji wa pembejeo kwa bei stahiki, hatua inayochangia kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

Mbali na mifumo hiyo, amesema taasisi za sekta ya kilimo zinaendelea kutumia huduma nyingine za e-GA, ikiwemo Government Email System na Mfumo wa Ofisi Mtandao, ambazo zimeongeza ufanisi wa mawasiliano na usimamizi wa shughuli za kila siku.
Ametoa wito kwa wananchi na wadau kutembelea banda la e-GA katika maonesho yanayoendelea jijini Dodoma ili kujionea mifumo mbalimbali ya kidijitali na namna inavyochangia kuboresha huduma katika sekta ya kilimo na maeneo mengine ya maendeleo.


