Na Mwandishi Wetu
UBALOZI wa Marekani nchini Tanzania leo 21 Mei 2026, umetangaza kuwa Serikali ya Marekani imemwekea vikwazo kwa kumzuia kuingia nchini humo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi Tanzania (SACP) Faustine Mafwele kwa madai ya kuhusika katika ukiukaji mkubwa wa Haki za Binadamu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio, Marekani imesema inazo taarifa za kuaminika zinazomuhusisha Mafwele na vitendo vya ukandamizaji pamoja na vitendo vya ukiukaji wa Haki za Binadamu.
Taarifa hiyo imesema vikwazo hivyo ni sehemu ya juhudi zake za kuwawajibisha watu wanaotuhumiwa kukandamiza haki za msingi za wananchi ambapo chini ya vikwazo hivyo Mafwele hatoruhusiwa kuingia Marekani.
Marekani imedai kuwa hatua hiyo imetokana na taarifa za uchunguzi zinazohusiana na matukio ya mwaka 2025, ambapo baadhi ya askari wa Jeshi la Polisi Tanzania waliwakamata, kuwatesa na kuwafanyia ukatili wanaharakati.
Wanaharakati hao ni Agather Atuhaire wa Uganda na mwanaharakati wa Kenya, Boniface Mwangi, walipokuwa jijini Dar es Salaam kufuatilia kesi ya uhaini inayomkabili kiongozi wa upinzani, Tundu Lissu.



