Na Mwandishi Wetu
KLABU ya Yanga imetozwa faini ya Sh 30 milioni kwa kosa la wachezaji na maofisa wa benchi la ufundi kukataa kutumia chumba rasmi cha kuvalia katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, badala yake kutumia nyumba iliyopo nje ya uwanja huo upande wa pili wa barabara.
Tukio hilo lilitokea Mei 3, 2026 wakati wa mchezo wa Derby ya Kariakoo dhidi ya Simba uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2.
Kwa mujibu taarifa ya Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Tanzania iliyotolewa leo Mei 11, 2026 na Bodi ya Ligi (TPLB), kitendo hicho ni ukiukwaji wa Kanuni za Ligi Kuu kuhusu taratibu za mchezo.
Mbali na adhabu hiyo, Yanga pia imepewa onyo kali baada ya kuchelewa kuwasili uwanjani kwa mchezo huo, ikifika saa 10:35 alasiri badala ya saa 10:30 alasiri kama kanuni zinavyotaka.
Katika hatua nyingine, Meneja wa Yanga, Walter Harson, amefungiwa michezo mitatu pamoja na kutozwa faini ya Sh milioni moja kwa kosa la kumsukuma mchezaji wa Simba, Clatous Chama, wakati wa mchezo huo.



