Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu, Dk.Mwigulu Nchemba, amehimiza ufungaji wa kamera nyingi katika viwanja vya michezo, ikiwamo uwanja Arusha ili kudhibiti vitendo vya ushirikina na imani potofu.
Amesema hayo leo Aprili 17, 2026, wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya katika uwanja wa Arusha utakaotumika kwa michuano ya AFCON 2027.
Amesema ni muhimu kuhakikisha kila eneo la uwanja linaonekana wazi, akieleza kuwa hata vitendo vidogo visivyofaa vinapaswa kubainika mapema kupitia mifumo ya ufuatiliaji.


“Uwanja uwe na kamera nyingi, hata mtu akiweka sindano aonekane ili tukomeshe ushirikina wa ndani ya viwanja, nuru iwe ndani na nje uwanja,” amesema. Pia Waziri Mkuu ametoa maagizo ya uharakishwaji wa mradi huo pamoja na matumizi stahiki ya fedha za ujenzi wa uwanja huo ili ukamilike, kuendana na muda wa maandalizi waliopewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).
“Kaguzi zitakuja mapema zaidi ya hapa. Fanyeni kazi usiku na mchana. Tusiweke dosari ambazo hazihusiani na maandalizi ya viwanja. Ongezeni vitendea kazi, ongezeni nguvu kazi ili tutekeleze mapema huo muda ambao tumeuweka.
“La pili tuendelee kuzingatia thamani na viwango vya fedha. Tutimize mahitaji na matakwa ya waendesha shughuli wa AFCON lakini lazima tuwape thamani ya viwango Watanzania ambao ndio watoa fedha ya ujenzi,” amesema Mwigulu.


