Na Mwandishi wetu, Dodoma
WAZIRI wa Madini, Anthony Mavunde, ameagiza kusimamishwa mara moja kwa shughuli zote za uchimbaji katika kijiji cha Busulwangili, wilayani Kahama, mkoani Shinyanga, ikiwa ni hatua ya kutatua mgogoro uliopo kati ya Kikundi cha Isunda, wamiliki wa mashamba pamoja na wamiliki wa maduara.
Maelekezo hayo yametolewa Aprili 14, 2026, jijini Dodoma katika ukumbi wa Tanzanite, Makao Makuu ya Madini, wakati wa kikao kilichowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta hiyo kwa lengo la kusikiliza hoja zao na kupata suluhisho la kudumu kuhusu uhalali wa umiliki na shughuli za uzalishaji.

Katika maelekezo yake, Waziri Mavunde amekiagiza Kikundi cha Isunda kusitisha mara moja shughuli za uchimbaji hadi kitakapowasilisha ndani ya siku tatu nyaraka muhimu, ikiwemo muhtasari wa kikao unaoonesha makubaliano ya wazi kuhusu haki ya kwanza ya uwekezaji kwa wamiliki wa maduara, kwa mujibu wa Kanuni ya 18A ya Sheria ya Haki za Madini.
Amefafanua kuwa kifungu hicho kinamtaka mwenye leseni, endapo ameanzisha wachimbaji wenye maduara na baadaye kupata mwekezaji mwingine, kuwapa kipaumbele cha kwanza wamiliki wa maduara kabla ya kuendelea na uwekezaji mwingine.

“Leseni ni kwa ajili ya uchimbaji pekee na siyo upangishaji. Ukiukwaji wowote wa taratibu hautavumiliwa,” alisisitiza Waziri Mavunde.
Aidha, ameeleza kuwa ni lazima kwa wamiliki wa leseni na maduara kuingia mikataba rasmi ya ushirikiano kabla ya kuanza shughuli za uchimbaji ili kuepusha migogoro ya mara kwa mara.
Katika hatua nyingine, Waziri huyo ameonya uongozi wa Kikundi cha Isunda dhidi ya kutoa taarifa zisizo sahihi zinazoweza kuchochea taharuki na migogoro miongoni mwa wachimbaji wadogo na wamiliki wa leseni.

Sambamba na hilo, ameiagiza Tume ya Madini Tanzania kutoidhinisha mikataba yoyote ya kiufundi hadi itakapojiridhisha kuwa hakuna mgogoro kati ya pande husika.
Ameongeza kuwa timu ya wataalamu itapelekwa katika kila duara kufanya tathmini ya uzalishaji, ukusanyaji wa mrabaha wa Serikali pamoja na kuhakikisha uwazi na uwajibikaji.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa, amesema kuwa suluhisho la kudumu la mgogoro huo linategemea majadiliano ya wazi yanayozingatia sheria, haki na maslahi ya pande zote.


