Na Mwandishi Wetu
RIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere imeanika mapungufu katika mchakato wa ununuzi na ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu jijini Arusha, unaojengwa kwa ajili ya mashindano ya fainali za Mataifa Afrika (AFCON).
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mradi huo unakosa thamani halisi ya fedha za umma kutokana na tofauti kubwa kati ya makadirio na thamani ya mkataba hali iliyoathiri maamuzi ya kibajeti na utekelezaji wa mradi.
Akizungumza wakati wa kuwasilisha ripoti hiyo leo Jumatatu Machi 30, 2026 kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Ikulu ya Dar es Salaam, Kachele amesema wakati mradi huo ukikadiriwa kugharimu shilingi bilioni 187, mkataba ulikuja kusainiwa kwa shilingi bilioni 338.54, likiwa ni ongezeko la asilimia 811.
“Mkandarasi alipatikana kwa njia ya mzabuni mmoja (single source) kwa kisingizio cha dharura bila kuwepo kwa Ushahidi wa hali hiyo. Hii iliondoa ushindani ambapo ingweza kuhakikisha upatikanaji wa bei nafuu na kulinda naslahi ya Serikali,” amesema.
Aidha amebainisha uwepo wa gharama zisizo halali, ikiwemo shilingi bilioni 3.27 zilizopachikwa kama gharama za zabuni, ambazo zilijumuishwa kwenye mkataba na kubebeshwa serikali. Hivyo kutoa mapendekezo kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuimarisha usimamizi wa ununuzi kwa kuhakikisha makadirio yanayoaminika na udhibiti madhubuti wa majadiliano ya mikataba.


