Na Mwandishi Wetu
MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, amesema deni la Serikali limeongezeka na kufikia sh. trilioni 110, hali iliyochangiwa na mikopo ya nje tofauti na mwaka wa fedha wa 2023/2024, ambapo deni lilikuwa chini ya kiwango hicho.
Akiwasilisha taarifa yake kwa Rais Samia Suluhu Hassan leo Jumatatu Machi 30, 2026 Ikulu ya Dar es Salaam, Kichere amesema hadi kufikia Juni 30, 2025 deni hilo limeongezeka kwa sh. trilioni 12.7, sawa na asilimia 13 ndani ya mwaka mmoja.
Kichere ameeleza kuwa kiasi hicho kinajumuisha deni la ndani la sh. trilioni 35.5 na deni la nje la sh. trilioni 74.55.
Ametaja sababu nyingine ya kuongezeka kwa deni la Serikali kuwa ni kushuka kwa thamani ya Shilingi ya Tanzania dhidi ya Dola ya Marekani, hali inayoongeza mzigo wa ulipaji wa deni la nje.
Hata hivyo CAG amefafanua kuwa “Tathmini ya uhimilivu wa deni imebaini kuwa deni la Serikali bado lipo ndani ya viwango salama vinavyokubalika Kimataifa huku thamani ya sasa ya deni lote la umma kwa pato la Taifa ikiwa ni asilimi 40.7 chini ya ukomo wa asilimia 55 na deni la nje kwa pato la Taifa likiwa ni asilimia 24.9 chini ya ukomo wa asilimia 40,”


