Na Mwandishi wetu
WANAFUNZI watatu wa Shule ya Msingi Msongola iliyopo eneo la Msongola, wilayani Ilala jijini Dar es Salaam, wamefariki dunia baada ya kupigwa na radi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amesema tukio hilo limetokea leo Machi 18, 2026 majira ya saa 5:00 asubuhi wakati wanafunzi hao wakiwa katika mazingira ya shule, ambapo radi hiyo ilisababisha vifo vya wanafunzi watatu na kujeruhi wengine wawili.
Amewataja waliopoteza maisha katika tukio hilo ni Alexander Paul, mwanafunzi wa darasa la tano, Ally Pongwe wa darasa la tatu pamoja na Hudhaifa Shafii, pia mwanafunzi wa darasa la tano.
“Aidha, wanafunzi wawili walijeruhiwa katika tukio hilo, ambao ni Nadri Maneno (8), mwanafunzi wa darasa la tatu, na Mahadi Ramadhan (8), mwanafunzi wa darasa la pili. Majeruhi hao waliwahishwa katika hospitali ya karibu kwa ajili ya kupatiwa matibabu na hali zao zinaendelea kufuatiliwa,” amesema Kamanda Muliro.
Katika tukio lingine, amesema Jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa mauaji ya Athumani Nyanza, ambaye mwili wake uligundulika ukiwa umefukiwa kwenye shimo karibu na nyumba yake, mtaa wa Kimya Kimya, Zingiziwa, wilayani Ilala.
“Jeshi la Polisi linatoa wito kwa wananchi waendelee kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa muhimu ili kuzuia matukio ya kihalifu,” amesema Kamanda Muliro.


