Na Mwandishi Wetu
SENEGAL imevuliwa ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 baada ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kubatilisha matokeo na kuwapa ubingwa huo Morocco.
Uamuzi huo ni kutokana na rufaa iliyowasilishwa na Shirikisho la Soka la Morocco (FRMF), ambapo CAF imesema imekubalika kisheria na imeamuliwa kwa faida yao.
CAF imewapa ushindi Morocco katika rufaa hiyo na ‘ushindi wa mezani’ wa mabao 3-0, hivyo Senegal kutakiwa kurejesha kombe na medali, ili wakabidhiwe mabingwa wapya, ambao sasa ni Morocco.
Maamuzi hayo yanaelezwa kuwa ni kutokana na Senegal kugomea mchezo kwa dakika kadhaa kutokana na Morocco kupewa penati iliyopigwa na Ibrahim Diaz.
Katika taarifa ya CAF imesema kuwa Senegal ilikiuka Kifungu cha 82 cha kanuni za AFCON, jambo lililosababisha kutumika kwa Kifungu cha 84.
Kifungu cha 82 kinaeleza kuwa ikiwa timu itakataa kucheza au itaondoka uwanjani kabla ya muda wa kawaida kuisha bila ruhusa ya mwamuzi, itachukuliwa kama imepoteza na itaondolewa kwenye mashindano.
Kifungu cha 84 kinaongeza kuwa timu yoyote itakayokiuka Kifungu cha 82 itaondolewa kabisa kwenye mashindano na kupoteza mechi hiyo kwa mabao 3-0.


