Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi mkoani Songwe linawashikilia watu saba, wakiwamo askari polisi wawili na madereva wa treni kwa tuhuma za kuhusika na wizi wa mifuko 534 ya mbolea aina ya Irea yenye thamani ya zaidi ya Sh 45 milioni.
Mbolea hiyo, mali ya kampuni ya Ocean Network ya nchini Zambia, ilikuwa inasafirishwa kwa njia ya reli kutoka Dar es Salaam kuelekea nchi jirani ya Zambia na kuibiwa usiku wa Agosti 19, 2025 katika Kijiji cha Nanyala, Wilaya ya Mbozi.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 2,2025, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Augostino Senga, amesema watuhumiwa hao wanashikiliwa kwa kushirikiana kupanga njama na kusimamisha treni yenye usajili wa namba 0139A mali ya TAZARA, katika eneo lisilo rasmi kwa ajili ya kushusha mbolea hiyo.
Amesema kuwa watuhumiwa hao ni pamoja na wafanyabiashara wa mbolea na askari hao wawili waliokuwa wakisindikiza treni hiyo.
“Katika msako uliofanyika, Polisi walifanikiwa kukamata mifuko 134 ya mbolea hiyo ikiwa imefichwa kwenye nyumba ya mmoja wa watuhumiwa katika Kijiji cha Ipoloti, Kata ya Bara, Wilaya ya Mbozi,” amesema.
Aidha ameeleza kuwa majina ya watuhumiwa hao yanahifadhiwa kwa ajili ya kipelelezi na uchunguzi wa kina unaendelea ili kubaini wahusika wengine na magari yaliyotumika kubeba mbolea hiyo.
“Hili ni tukio la kihalifu linalohusisha mtandao mpana wa watu hivyo tunafanya uchunguzi wa kina na tutahakikisha wote waliohusika wanafikishwa kwenye vyombo vya sheria,” amesema Kamanda Senga.