Na Winfrida Mtoi
Msanii wa Bongo Flava, Frank Humbuchi maarufu Foby amewataka watanzania na wasanii wenzake kuichangia timu ya Taifa ya Soka kwa watu wenye ulemavu ‘Tembo Warriors’ ili kuiwezesha kushiriki Mashindano ya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA)yatakayoanza Septemba 8 -14, 2025 nchini Burundi.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 1, 2025, jijini Dar es Salaam, Foby amesema ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha anaiwezesha timu hiyo kushiriki mashindano hayo kama wanavyofanya katika timu nyingine.

“Niwaombe wasanii wenzangu tusapoti vitu vya kwenye nchi yetu, naomba tuchangie timu yetu tusisubiri kupigiwa simu, tujaribu kusapoti kwenye hili jambo. Sisi ndio tunaweza tukasimama sehemu tukawashawishi watu kufanya jambo na wakaitika,’ amesema.
Akizungumzia hali ya michango ilipofikia tangu wameanza kuchangisha Agosti 15, 2025 kupitia lipa namba, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Shirikisho la Soka kwa Watu Wenye Ulemavu Tanzania (TAFF), Abdul Mashine, amesema wamekusanya sh 270, 000 kati ya milioni 73 wanazohitaji.
“Tumeandaa lipa namba kwa ajili ya Watanzania kuchangia, lengo ilikuwa kupata watanzania milioni moja ambao kila mmoja akichangia shilingi 100 tutakusanya shilingi milioni 100 ambazo tulitaka kuzitumia kwa timu mbili ya wanaume na wanawake. Tangu tarehe 15 tulivyoanza kukusanya hadi sasa tumefanikiwa kukusanya shilingi 270,000,”
Hata hivyo ameeleza kuwa mashindano kwa timu za wanawake yameahirishwa ambapo kwa sasa wanahitaji kiasi cha sh 73 milioni kwa ajili ya kikosi cha wanaume pekee.
Amesema Serikali kupitia Baraza la Michezo la Taifa wamewaahidi kuwapa tiketi za ndege za kwenda na kurudi, lakini changamoto iliyopo ni kupata fedha ya mchango wa ushiriki ambayo ni Dola 4000, itayogharamia malazi na mambo mengine wakiwa nchini Burundi.