Na Mwandishi Wetu
Rais Samia Suluhu Hassan, amezindua rasmi Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ambapo ametoa wito kwa taasisi za umma na sekta binafsi ili kufanikisha utekelezaji wa malengo ya dira hiyo.
Akihutubia katika hafla ya uzinduzi huo uliofanyika leo Julai 17,2025 jijini Dodoma, Rais Samia, ameiagiza Tume ya Taifa ya Mipango kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu kuandaa mifumo ya kupima utekelezaji wa dira hiyo kwa vitendo ili kuhakikisha inaleta matokeo chanya kwa wananchi.
Rais Samia ametaka watu kubadili mitazamo na kuacha kufanya kazi kwa mazoea na kuzitaka wizara kubadilisha sera zao kuhakikisha zinaendana na utekezaji wa dira hiyo, ikiwamo kupimana kwa matokeo ya kazi.

Aidha amezitaka sekta binafsi kujipanga vema katika kushiriki utekelezaji huo katika maeneo yote ya kiuchumi kwa kuwa ndiyo mhimili wa ujenzi wa uchumi waTaifa ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa shabaha ya dira hiyo.
“ Utekelezaji wa Dira 2050 unahitaji ushiriki wa dhati na wa kimkakati, kutoka kwa sekta binafsi katika maeneo yote ya kiuchumi, uwekezaji, ubunifu na uundwaji wa ajira zenye staha,” amesema.

Amefanunua kuwaserikali ya sasa imejikita katika kupanua uchumi jumuishi kwa kuwalenga watu wa kada zote, kutoka mijini hadi vijijini, huku ikiendelea kukuza uchumi, kuwezesha wanawake na vijana, na kushirikisha sekta binafsi pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.
Amebainisha kuwa Dira 2050 ni matokeo ya fikra, maono na matakwa ya watanzania wenyewe kuelekea maendeleo endelevu, huku akisisitiza usawa uwajibikaji na ushirikishwaji wa wananchi wote.
Katika hatua nyingine Rais Samia amesifu utendaji wa Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango katika nafasi mbalimbali alizotumikia Taifa na kusisitiza kuwa hatapumzika kwa sababu usimamizi wa dira na mipango ya maendeleo ni jukumu lake.

“Mheshimiwa Dk Mpango ni gwiji wa mipango ya maendeleo katika nchi hii, alishiriki katika kuandaa Dira 2025, alishiriki kuandaa Program ya Big Result Now (BRN) alikuwa katibu mkuu wa Tume ya Mipango iliyovunjwa na baadaye waziri wa iliyokuwa Wizara ya Fedha na Mipango.
‘Tunathamini sana mchango wako Mheshimiwa Makamu wa Rais katika nafasi zote ulizozifanyia kazi. Kwa maana hiyo kama mnakumbuka Dk. Mpango alisema kwa anavyojisikia angeomba kupumzika, lakini nilikuwa namwambia hupumziki, usimamizi wa dira na mipango ya maendeleo ni jukumu lake kwa hiyo atapumzika kiaina lakini yupo kazini,’ ameeleza.
Naye Dk. Mpango amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo inachochea matumaini ya wananchi na kutoa maamuzi ya kisera na kaunda maendeleo ya nchi.

Amesema kutokana na vijana kuwa rasilimali yenye nguvu nchini ni muhimu kuwekezea elimu ya dira hiyo mpya kwa vijana kuamsha fikra bunifu kwa vijana hao.
Kwa upande wake Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo amesema moja ya malengo ya dira hiyo ni kuifanya Tanzania ifikie hadhi ya uchumi wa kipato cha kati ngazi ya juu ambao utafanya pato la Taifa kwa Mtu mmoja kufikia Sh 18 milioni kwa mwaka au 1.52 milioni kwa mwezi.
Profesa Mkumbo amesema kwa sasa pato la mtanzania ni milioni tatu kwa mwaka.
“Shabaha nyingine ni Tanzania kuwa Mzalishaji mkuu wa chakula barani Afrika na miongoni mwa nchi kumi bora duniani, mtanzania kuishi wastani wa miaka 75 yenye afya na furaha, Watoto wote wa kike na wa kiume wana fursa sawa ya malezi bora ya utotoni, huku angalau asilimia 90 ya watoto wote wakiwa katika hatua sahihi za ukuaji unaoonesha uwezo wao kamili ifikapo umri wa miaka mitano,” amesema Prof. Mkumbo.