Na Mwandishi Wetu
Kuelekea pambano la ngumi la ‘Dar Boxing Derby’, bondia Karim Mandonga kama kawaida yake, ametambulisha ngumi mpya atakayompigia mpizani wake Shaban Kaoneka inayoitwa Kilumbilumbi.
Akizungumza wakati wa utambulisho wa mabondia watakaopanda ulingoni siku ya pambano hilo Julai 26, 2025 kwenye viwanja vya Leaders Club jijini Dar es Salaam, Mandonga ametamba kuwa ngumi hiyo ina madhara makubwa tofauti na zote alizowahi kutumia ulingoni.
” Kama mnavyojua kila ngumi inakuja na slogan, nilikuja na ndoinge, tukaja na pelesupelesu na sugunyo. Niwaambie tu kuwa ngumi ya sasa inaitwa Kilumbilumbi, ina madhara sana maana Kaoneka akikutana nayo inafuta kumbukumbu zote katika ubongo wake,” amejitapa Mandonga.

Pia amempa jina jipya mpinzani wake kuwa anaitwa Kaonewa badala ya Kaoneka kwa sababu licha kushinda mechi iliyopita lakini Mandonga aliyepigwa ndiye aliyepata umaarufu na utajiri.
” Huyu haitwi Shabani Kaoneka, naitwa Shambani Kaonewa, kama mara ya kwanza aliweza kunipiga halafu nikawa tajiri mara hii atakuwa nani huyo. Huyu safari hii ninampiga kwanza sina njaa, natembelea gari ya kifahari tofauti na kipindi kile,” ametamba Mandonga.
Kwa upande wake Kaoneka amesema kipindi hiki anaingia akiwa na uongozi mpya na lazima atampiga kwa mara nyingine Mandonga atake asitake.

Pambano kubwa siku hiyo litamkutanisha Ibrahim Class ‘King Class’ dhidi ya Nasibu Ramadhani ambao wote kila mmoja ametamba kummaliza mapema mpinzani wake.
Bondia King Class ambaye alifika katika utambulisho huo viwanja vya Mabibo akiwa na msafara uliongozwa na gari ya Polisi, amesema pamoja na mpizani wake kutamba lakini atambue anakwenda kumchapa kama zaidi ya kipigo alichompa katika pambano la kwanza walipokutana.

Naye Nasibu ameeleza kuwa mara nyingi Class huwa anabebwa na waamuzi lakini safari hii amemhakikishia kuwa hawezi kukubali tena unyonge.
” Kushindwa mara moja si kama utashindwa siku zote na ukiangalia pambano analosema kanipiga ni miaka kadhaa imepita kwa sasa kuna mabadiliko makubwa, nimeshacheza mechi nyingi ngumu. Nadhani tarehe 26 ndio siku yake ya kupotea,” ametamba Nasibu.

Zaidi ya mapambano 15 yatapigwa siku hiyo baadhi wengine watakaopanda ulingoni ni Said Toress atazichapa na Baraka Mazola, Viguro Shafii dhidi ya Idd Pazi, Hamad Furahisha atamvaa Japhet, Khalid Karama na Black Cobra, Said Mwanga dhidi la Loren Japhet.
Wengine ni Adam Peter atazichapa na Abdallah Pombe, John Chuwa na Jamal Kunoga, Ramadhani Shauri dhidi ya Issa Nampepeche, wakati wanawake ni Debora Mwenda na Asia Meshack, Stumai Muki atapigana na Sara Alex.