Na Mwandishi Wetu
Kocha Mkuu wa Yanga, Miloud Hamad amesema hawaandai wachezaji wake kisaikolojia kwa sababu si wagonjwa, wako vizuri kiakili, yeye kama kocha kazi yake ni kuwaandaa kimbinu na kuwa fiti
Miloud ametoa kauli hiyo, leo Juni 17, 2025 kuelekea mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Tanzania Prisons unatarajiwa kupigwa kesho, kwenye Uwanja wa Sokoine, jijini Mbeya.
Kocha huyo ametamba kuwa wana fainali nne za kucheza na mojawapo ni mchezo huo na Prisons, wamejiandaa vizuri kukabiliana na wapinzani wao kuhakikisha wanapata ushindi.

“Maandalizi yetu yapo vizuri sana, tuna fainali nne za kucheza. Tupo tayari kuukabili mchezo wa kesho kikamilifu. Kila mchezaji anajua kitu gani cha kufanya kesho, kikosi chetu kipo kamili hakuna majeruhi wapya. Hatuna presha yoyote na hatuna sababu ya kuwa na presha.
“Tunaheshimu sana Tanzania Prisons, lakini sisi ni Yanga. Nina wachezaji wenye uzoefu na uwezo mkubwa. Tunajua utakuwa mchezo mgumu lakini hatuna sababu ya kuwaza sana kuhusu hilo. Tumekuja kushindana kwa tahadhari kubwa,” amesema kocha huyo.

Aidha amewashukuru mashabiki wa timu hiyo kwa sapoti yao kubwa kwa kuwa amefanya kazi na klabu nyingi lakini wa Yanga wamekuwa tofauti kutokana na kujitoa kila sehemu timu inapokwenda.
“Tumekuja Mbeya kusaka alama tatu tunawashukuru sana mashabiki, nimefanya kazi Klabu mbalimbali kubwa lakini mashabiki wa Yanga ni mashabiki wa mfano. Naamini kesho kwa mchango wao Uwanjani basi tutakuwa na wakati mzuri. Niwaombe sana mashabiki wajitokeze kwa wingi,”
Kwa upande wake kocha wa Tanzania Prisons, Amani Josiah amesema wamejiandaa kucheza na timu ambayo iko imara, lengo lao ni kutumia faida ya kucheza nyumbani kuepuka kucheza mechi za mtoano ‘play off’
Amesema kutakuwa na mabadiliko kimbinu kulingana na aina ya timu wanayokutana nayo, pia hawana majeruhi katika kikosi chao ambapo wachezaji waliokosekana kwa muda mrefu tayari wamerejea.