Na Mwandishi Wetu
Serikali imetoa wito kwa wananchi kubadilika na kuwekeza katika bima ya afya kama njia ya kujiandaa na changamoto za kiafya, ikiwemo gharama kubwa za matibabu ya magonjwa kama saratani.
Wito huo umetolewa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel, leo Juni 12, 2025 alipokuwa akijibu swali la nyongeza kutoka kwa Ester Matiko (Viti Maalum), ambaye alitaka kufahamu kama Serikali haioni haja ya kuweka kifurushi cha saratani kwenye bima ya afya ya chini ili kuwezesha wananchi wa kawaida kupata huduma, kutokana na gharama kubwa za matibabu ya ugonjwa huo.
Akijibu swali hilo, Dk. Mollel amesema jamii inapaswa kubadilika na kuwekeza kwenye bima ya afya ili kuimarisha afya zao.
“Watu wako tayari kuchangisha milioni 100 kwa ajili ya harusi, lakini mtoto anapozaliwa hakuna anayechangia hata kwa ajili ya matibabu. Hii inaonyesha kwamba jamii inathamini sherehe kuliko afya,” amefafanua Dk. Mollel.
Aidha, Dk. Mollel amebainisha kuwa Serikali imetenga zaidi ya Sh 200 bilioni kwa ajili ya msamaha wa matibabu, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha wananchi, hususan wasio na uwezo, wanapata huduma za afya bila vikwazo vya kifedha.
Naibu Waziri amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mifumo ya bima ya afya ili kuhakikisha huduma za afya, zikiwemo za magonjwa yasiyoambukiza kama saratani, zinapatikana kwa wote kwa gharama nafuu kupitia mfumo wa bima ya afya kwa wote unaotarajiwa kuimarika zaidi katika utekelezaji wa sera mpya ya afya.
Katika hatua nyingine amesema Serikali inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kukabiliana na ongezeko la wagonjwa wa saratani nchini, ikiwemo kuimarisha huduma za kinga, uchunguzi wa awali na matibabu ya ugonjwa huo hatari.
Akijibu swali la Mariam Nassoro Kisangi (Viti Maalum) aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani wa kudhibiti ongezeko la wagonjwa wa saratani nchini.
Dk. Mollel amesema Serikali imeanzisha na kuimarisha mikakati kadhaa ya mapambano dhidi ya ugonjwa huo hatari, ikiwemo utoaji wa elimu kwa umma kuhusu namna ya kujikinga.
“Tunatoa elimu kupitia redio, televisheni, magazeti, machapisho na mitandao ya kijamii ili kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwajengea uelewa juu ya kinga dhidi ya saratani.
“Pia, Serikali inaendelea kutoa chanjo ya HPV kwa wasichana kwa lengo la kuwalinda dhidi ya virusi vinavyosababisha saratani ya mlango wa kizazi, ambayo ni miongoni mwa saratani zinazowaathiri wanawake wengi nchini,’ amesema.
Aidha amesema Serikali imeimarisha huduma za uchunguzi wa awali na matibabu ya saratani katika ngazi zote za huduma za afya kuanzia zahanati, vituo vya afya hadi hospitali za mikoa na Taifa.
“Tumewapatia wataalamu mafunzo maalum na pia kuweka vifaa tiba muhimu katika hospitali mbalimbali nchini kwa ajili ya kutoa huduma za kibingwa kwa wagonjwa wa saratani,” ameongeza.