Na Mwandishi Wetu
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Geophrey Pinda amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kukabiliana na migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji katika maeneo mbalimbali hapa ikiwemo Mkoa wa Morogoro.
Ametoa kauli hiyo bungeni jijini Dodoma leo Juni 6, 2025 wakati akijibu swali la Dk. Christine Ishengoma Mbunge wa Vitu Maalum, aliyeuliuza ni upi mkakati wa Serikali wa kumaliza migogoro ya wakulima na wafugaji mkoani Morogoro?
Amesema hatua nyingine walizozichukua ni kupitia mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) ambapo miji chipukizi kama ilivyo kwa miji ya halmashauri hupangwa, hupimwa na humilikishwa sambamba na kuweka mipango ya matumizi bora ya ardhi.
“Serikali inatambua kuwepo kwa migogoro ya wafugaji mkoani Morogoro, hata hivyo serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kukabiliana na migogoro hiyo ambapo baadhi ya hatua hizo ni mipango ya matumizi bora za vijiji ili kubainisha maeneo ya kilimo sambamba na maeneo ya wafugaji kupitia Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi,” amesema Pinda.
Aidha, Naibu Waziri Pinda ametoa rai kwa wananchi kuhakikisha wanatumia ardhi kuendana na mipango ya matumizi iliyopangwa ili kuondoa muingiliano wa matumizi ya ardhi ambayo imekuwa chanzo cha migogoro ya wakulima na wafugaji.