Na Tatu Mohamed
SHIRIKA la The Foundation of Civil Society (FCS) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa kimataifa, limetangaza kufanyika kwa Wiki ya Azaki itakayofanyika jijini Arusha kuanzia Juni 2 hadi 6, 2025.
Wiki ya Azaki, ambayo imekuwa ikiadhimishwa kila mwaka, inalenga kujadili masuala mbalimbali ya kijamii na maendeleo.

Kwa miaka ya hivi karibuni, tukio hili limekuwa jukwaa muhimu linalowakutanisha watu kutoka makundi tofauti ili kuangazia masuala ya maendeleo.
Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa FCS, Justice Rutenge, amesema tukio la mwaka huu litaunganisha wadau wa maendeleo kutoka pande mbalimbali kwa ajili ya kujadili njia mbalimbali za kufanikisha maendeleo endelevu.

“Wiki ya Azaki itajikita katika kujadili njia za kuelekea kwenye dira ya taifa ya maendeleo. Tutakuwa na mijadala mingi kuhusu masuala ya msingi kama kukuza ujasiriamali, demokrasia nchini, na ubia katika maendeleo,” amesema Rutenge.
Nesia Mahenge, Mwenyekiti wa Kamati ya Azaki nchini na Mkurugenzi Mkazi wa CBM (Christian Blind Mission), ameeleza kuwa tukio hili ni fursa ya pekee kwa watu kutoka sekta mbalimbali kujifunza na kuchangia maendeleo ya kitaifa.“Tunashirikiana kwa karibu na serikali ili kuhakikisha mjadala huu wa maendeleo unaongozwa vyema,” amesema Mahenge.

Wiki ya Azaki mwaka huu imewezeshwa na mashirika mbalimbali ya kijamii na kifedha. Doreen Dominic kutoka Benki ya Stanbic, ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Taasisi za Umma na Mashirika Binafsi, amesema ushiriki wao unalenga kuchochea maendeleo ya jamii.
“Stanbic Bank Tanzania ni mdhamini rasmi wa Wiki ya Azaki 2025 kwa mchango wa shilingi milioni 40. Pia tutatoa elimu ya fedha kwa mtu mmoja mmoja, mashirika, na wajasiriamali,” amesema Dominic.

Aidha, Ismail Biro, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa asasi ya Tanzania Bora, ametoa wito kwa wadau wote wa maendeleo kuthibitisha ushiriki wao kwenye tukio hilo.
