Na Mwandishi Wetu
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imemhukumu mfanyabiashara, Hamis Luwongo, kunyongwa hadi kufa baada ya kupatikana na hatia ya kumuua mke wake, Naomi Marijani.
Uamuzi huo umetolewa leo Februari 26, 2025 na Jaji wa Mahakama hiyo, Hamidu Mwanga, baada ya kuridhishwa na ushahidi wa mashahidi 14 na vielelezo 10 uliotolewa mahakamani hapo.

Kabla ya kutolewa kwa adhabu hiyo, jopo la mawakili wawili wa Serikali ukiongozwa na Wakili Mkuu wa Serikali, Yasinta Peter akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Ashura Mnzava, uliomba Mahakama itoe adhabu kali dhidi yamshtakiwa huyo ili iwe fundisho kwa wanaume wote wanaowafanyia ukatili wanawake wao kwa kigezo wapo kwenye ndoa.
Katika kesi hiyo ya jinai namba 44/2023, Hamis, mkazi wa Gezaulole, wilayani Kigamboni, alikuwa anakabiliwa na shtaka la mauaji ya mkewe Naomi Orest Marijani kinyume cha kifungu cha 196 na 197 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, kama ilivyorejewa mwaka 2019.
Anadaiwa kutenda kosa hilo Mei 15, 2019 nyumbani kwao kisha akauchoma mwili kwa kutumia magunia mawili ya mkaa ndani ya banda la kuku.
Inadaiwa masalia ya mwili na majivu alikwenda kuyazika shambani na kupanda migomba juu yake.