Na Winfrida Mtoi
Baraza la Mtihani la Tanzania (NECTA), limewataka wamiliki na wakuu wa shule kutambua kuwa shule zao ni vituo maalumu vya mitihani, hivyo hawatakiwi kuingilia majukumu ya wasimamizi.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mtendaji wa NECTA, Dk. Said Ally Mohamed leo Septemba 10,2024 mbele ya waandishi wa habari wakati akitangaza idadi ya watahiniwa wa darasa la saba waliosajiliwa kufanya mtihani wa kumaliza Elimu ya Msingi unaoanza kesho Septemba 11 hadi Septemba 12,2024.
Dk. Mohamed amesema Baraza hilo halitasita kukifuta kituo chochote cha mtihani endapo litajidhihirisha uwepo wake unahatarisha usalama wa mitihani ya Taifa.
“Wakuu wa shule watatekeleza majukumu yao ya usimamizi kwa kuzingatia mwongozo wa usimamizi uliotolewa na Baraza la Mitihani na kuepuka kuingilia usimamizi wa watahiniwa ndani ya vyumba vya mitihani,” amesema.
Akitaja idadi ya watahiniwa walisajiliwa kufanya mtihani huo kwa Tanzania Bara, Dk. Mohamed amesema ni 1,230,780, wavulana 564,176 sawa na asilimia 45.84 na wasichana wakiwa ni 666,604 sawa na asilimia 54.16 kutoka katika shule 18,964.
Amefafanua kuwa kati ya watahiniwa hao, 1,158,862 watafanya mtihani kwa Lugha ya kiswahili na 71,918 watafanya kwa Kiingereza, lugha ambayo walikuwa wanatumia katika kujifunza.
Aidha alitaja watahiniwa wenye mahitaji maalumu waliasajiliwa kufanya mtihani huo kuwa ni 4,583, kati yao 98 ni wasioona, 1,402 wenye uoni hafifu, 1,067 wenye uziwi, 486 wenye ulemavu wa akili na 1,530 ni wenye ulemavu wa viungo.
Ameeleza kuwa mtihani huo utakuwa na jumla ya masomo sita ambayo ni kiswahili, Kiingereza/ ,English Languege” Sayansi na Teknolojia, Hisabati, Maarifa ya Jamii na Stadi za Kazi na Uraia na Maadili.