HALI ya miundombinu katika mikoa ambayo imepitiwa na mvua za el nino ni mbaya. Barabara nyingi, hasa za changarawe na udongo, zina hali mbaya sana. Hata za lami kuna sehemu zimeharibika, yakiwamo madaraja madogo na makubwa. Hali kwa ujumla ni mbaya.
Katika jiji la Dar es Salaam ambalo kulingana na sensa ya watu na makazi ndilo bado linaongoza kwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya watu nchini, hali ni mbaya zaidi. Kwa mujibu wa ripoti ya Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022, Dar es Salaam ndiyo mkoa unaoongoza kwa idadi ya watu ukiwa na wakazi 5,383,728 ukifuatiwa na mkoa wa Mwanza wenye wakazi 3,699,872.

Hapana shaka, hata mchango wa mikoa kwa uchumi wa taifa unafungamana sana na wingi wa watu ambao huakisi pia shughuli za kiuchumi hasa kwa wale wanaoishi maeneo ya mijini.
Hakuna ubishi kwamba nguvu kubwa sana ya fedha itahitajika kurudisha miundombinu iliyoharibika katika hali yake ya awali, ili kusaidia mawasiliano. Lakini kubwa ni kurejesha shughuli za kiuchumi katika hali yake ya kawaida.
Yapo baadhi ya maeneo watu wamepoteza wapendwa wao, nyumba zao, mashamba yao na mali nyingi kutokana na athari za mvua hizi ambazo zimesababisha mafuriko katika maeneo mengi ya nchi hii. Nawapa pole wote waliopoteza wapendwa wao na mali zao pia.
Inaeleweka kwamba mvua za kupitiliza kiasi ni maafa. Hakuna mtu anayeandaa maafa ya asili kama mafuriko. Hizi ni kudra za Mwenzi Mungu. Hata hivyo, binadamu kwa kutumia maarifa ya kisayansi ana uwezo wa kupunguza kiwango cha madhara ya maafa haya. Hii ni pamoja na kuwa na taarifa sahihi na kuchukua hatua za tahadhari kwa wakati.
Kwa mfano, ingeliwezekana kabisa kuwaondoa kwa nguvu watu wote waliojenga na kuishi mabondeni, kwenye kingo za mito na maeneo yote ambayo kwa asili ni mapito na mkusanyiko wa maji – mabwawa.
Pamoja na uwezo huo, pia kuna suala la ubora wa ujenzi miundombionu yetu. Kwa mfano mpaka leo ni vigumu kuelewa inakuwaje mhandisi anajenga barabara isiyo na mitaro ya kuondosha maji ya mvua barabarani? Inakuwaje mhandishi wa ujenzi wa barabara anapitisha barabara mtoni kabisa yanakopita maji ya mto? Inakuwaje kwa mfano miaka na miaka, mafuriko yatokee sehemu ile ile, lakini wenye wajibu wa kuepusha hali hiyo kwa kubuni miundiombinu bora zaidi hawafanyi lolote?
Nitaje mkoa wa Dar es Salaam kama mfano – eneo la Jangwani. Hivi ni nani asiyejua kwamba kwa mpango na utekelezaji haitawezekana tena eneo lile kuwa salama kwa wakazi wa jiji hilo wakati wa mvua? Ni dhadhiri kwa zaidi ya miaka 10 sasa imekwisha kuthibitika kuwa pale Jangwani kunahitajika suluhisho la maana la kitaalam.
Kwamba hakuna sababu hata moja ya magari na hata waenda kwa miguu kwenda mpaka kwenye ukingo wa mto Msimbazi ndipo wavuke. Haitawezekana. Imethibitika kuwa hilo kwa sasa halitawezekana tena. Lakini ni nani anayewaza kama pale Jangwani palipaswa pawe pameshajengwa daraja kubwa kuanzia Magomeni mpaka Fire?

Tatizo kubwa la nchi yetu ni uwajibikaji. Yaani wakubwa wanaweza kufanya maamuzi ya ajabu sana, wakatumia mabilioni ya fedha za umma kutekeleza mradi mkubwa ambao haukufanyiwa tathmini ya kutosha juu ya uimara wake na uhimilivu kutokana na madhara mengine ya kimazingira.
Ni katika ‘ulevi’ wa ukubwa kama huo tulishuhudia karakana kuu ya mabasi ya mwendo kasi ikijengwa Jangwani. Yaani mtoni kabisa! Na madhara yalipotokea kwa mabasi mengi kujaa maji baada ya karakana hiyo kufurika maji, hakuna aliyewajibika. Hakuna.
Ni katika ‘ulevi’ wa ukubwa kama huo tulishuhudia karakana kuu ya mabasi ya mwendo kasi ikijengwa Jangwani. Yaani mtoni kabisa! Na madhara yalipotokea kwa mabasi mengi kujaa maji baada ya karakana hiyo kufurika maji, hakuna aliyewajibika. Hakuna.
Ukitembea kwenye barabara nyingi za nchi hii, suala la utaalam katika ujenzi wa barabara halizingatiwi kabisa. Barabara zinajengwa mpaka mtoni, mitaro ya maji ya mvua inaachwa kujengwa, kwenye miinuko mikali inaachwa hivyo hivyo, kwenye kona hatarishi vivyo hivyo.
Ipo mifano hai mingi tu. Jaribu kufikiria barabara kuu ya nchi hii, Barabara ya Morogoro, ile kona pale Kimara Mwisho mara tu baada ya kituo cha mabasi ya BRT, ni ya nini? Nini kilizuia kunyoosha ile barabara na kuepusha kero na hatari ya kona ile? Kulikuwa na gharama gani ya kushindikana kubebeka ili barabara pale inyooshwe? Hao wahandisi waliopitisha hiyo michoro walisahau kuwa hiyo barabara ndiyo inabeba malori karibu yote yanayotoka na kuingia bandari ya Dar es Salaam?
Hakuna anayeweza kuelewa kwamba wahandisi wetu wanasoma kanuni zile zile za ujenzi kama wa nchi nyingine, lakini wanapokuja kutekeleza kazi zao, wanaamua kupigwa ‘upofu’ kiasi cha kusahau kabisa misingi ya ubora wa kazi zao.
Kuna mtu mmoja alitoa ushuhuda mahali akisema, siyo kila masikini ni mtu mvivu. Wapo wanaofanya kazi kwa nguvu sana, lakini hawajikwamui walipo kwa sababu wamejifunga katika mnyororo fulani. Inahitajika nguvu kubwa ya kumsukuma huyo masikini hapo alipo ili ajikwamue. Fikiria jamaa anayejenga nyumba ya miti na udongo kila mwaka.
Fikiria kazi ya kwenda kukata miti, kuibeba, kujenga, kuikandika, lakini masika ikinyesha tu mchwa wananza kazi yao na mara nyumba yake ya miti inaanza kuegema upande kwa sababu haikujengwa kwenye msingi.

Je, ingelikuwa kuwa huyu jamaa amejenga nyumba yake kwenye msingi bora, wenye semeti, ni dhahiri nyumba yake ingelidumu muda mrefu zaidi na hasingelikuwa na kazi ya kujenga nyumba kila mwaka. Muda wake mwingine angeuelekeza kufanya mambo mengine ya maendeleo kama kujilimia chakula cha kutosha na ziada kuuza. Kidogo kidogo angepunguza umasikini wake.
Sisi kama taifa kwa kushindwa kufuata misingi bora ya ujenzi wa barabara na miundombinu mingine, tunajikuta mwaka baada ya mwaka tukiwa pale pale tukishughulika na jambo lilelile kwa gharama kubwa. Hatupigia hatua. Tunajifunga kwenye mnyororo wa umasikini, kwa kupuuza tu kanuni za ujenzi.
Jaribu kufikiria eti pale Jangwani siku hizi kuna mitambo ya ujenzi – vijiko, mAgreda, ambayo imepiga kambi wakati wote kusubiri kutoa mchanga na matope wakati wa mafuriko. Hivi ile mitambo pale ni ya nani? Nani analipa gharama zake? Kwa nini imekuwa ni kazi ya kudumu? Kwa nini barabara ile isifumuliwe na kunyanyuliwa juu ili kuepuka yale maigizo ya kujilipa fedha za umma kwa kundoa mchanga mtoni? Umasikini mwingine tunajitakia wenyewe!
Jaribu kufikiria eti pale Jangwani siku hizi kuna mitambo ya ujenzi – vijiko, magreda, ambayo imepiga kambi wakati wote kusubiri kutoa mchanga na matope wakati wa mafuriko. Hivi ile mitambo pale ni ya nani? Nani analipa gharama zake? Kwa nini imekuwa ni kazi ya kudumu? Kwa nini barabara ile isifumuliwe na kunyanyuliwa juu ili kuepuka yale maigizo ya kujilipa fedha za umma kwa kundoa mchanga mtoni? Umasikini mwingine tunajitakia wenyewe!