Na Mwandishi Wetu
UBUNIFU wa mfumo jumuishi wa kuhifadhi mazao kwa kutumia teknolojia ya ubaridi umeibuliwa na mwalimu wa Chuo cha Elimu ya Ufundi Stadi (VETA) Kihonda, Mwalimu Masumbuko Maliganya, kwa lengo la kuwasaidia wakulima, wafugaji na wafanyabiashara kupunguza hasara zinazotokana na kuharibika kwa bidhaa zao.
Maliganya, ambaye ni mwalimu wa fani ya Refrigeration and Air Conditioning, alisema mfumo huo wa cold room umebuniwa ili kutoa suluhisho kwa wakulima wa mbogamboga, matunda na mazao mengine ambao mara nyingi hulazimika kuuza kwa bei ndogo kutokana na wingi wa mazao sokoni au kuyapoteza yanapokaa muda mrefu.

Alisema teknolojia hiyo ina uwezo wa kuhifadhi mbogamboga kwa zaidi ya wiki tatu, hivyo kumpa mkulima nafasi ya kusubiri wakati mzuri wa bei kabla ya kuuza mazao yake.
“Nimefikiria namna ya kumsaidia mkulima ambaye amezalisha kwa wingi lakini bei iko chini. Kupitia cold room hii anaweza kuhifadhi mazao yake hadi pale soko litakapokuwa zuri na kupunguza hasara,” alisema.
Alieleza kuwa mfumo huo pia unaweza kutumika na wafanyabiashara wadogo, hususan wanawake wanaouza mbogamboga, matunda, maziwa na bidhaa nyingine zinazoharibika haraka.
Kwa mujibu wake, teknolojia hiyo inaweza kusaidia kuanzisha dhana ya “genge janja”, ambapo muuzaji anaweza kuhifadhi bidhaa zake katika mazingira salama na kuendelea kuuza bila hofu ya mazao kuharibika au kupunguza bei kwa hasara.

Aidha, alisema cold room hiyo imegawanywa katika sehemu maalumu zinazowezesha kuhifadhi bidhaa mbalimbali ikiwemo nyama, maziwa, samaki, vinywaji pamoja na mazao ya shambani.
Maliganya alisema ubunifu huo ni sehemu ya mchango wa wataalamu wa ufundi katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi na kuongeza thamani ya uzalishaji wa ndani.
Alisema matumizi ya teknolojia hiyo yatawezesha wakulima na wafanyabiashara kuongeza kipato, kupunguza upotevu wa chakula na kuchangia ukuaji wa sekta ya kilimo na mifugo nchini.


