📌 Aahidi kutumia jukwaa lake kuhamasisha wananchi kutumia umeme kwa shughuli za kupikia
📌 Ushirikiano huo waunga mkono jitihada za TANESCO na Serikali za kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia
Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
Mwanahabari nguli Maulidi Kitenge, ameungana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia kwa umeme, hatua inayolenga kuongeza uelewa wa jamii kuhusu faida za matumizi ya umeme jikoni na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanatumia nishati safi ya kupikia.
Maulidi amejiunga na kampeni hiyo baada ya kutembelewa na Uongozi wa TANESCO Kinondoni Kaskazini Julai 8, 2026, na kupatiwa elimu kuhusu matumizi ya umeme kwa shughuli za kupikia pamoja na mafunzo ya vitendo ya matumizi ya majiko ya umeme.

Mafunzo hayo yalitolewa na Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO Kinondoni Kaskazini, Bw. Juma Msuya, ambapo Maulidi alieleza kuvutiwa na urahisi, usalama na ufanisi wa matumizi ya umeme kwa shughuli za kupikia, na kuahidi kutumia jukwaa lake kuhamasisha wananchi wengi zaidi kuanza kutumia nishati hiyo.
Akizungumza baada ya mafunzo hayo, Meneja wa TANESCO Kinondoni Kaskazini, Mha. Godlove Mathayo, amesema ushirikiano na watu mashuhuri ni sehemu ya mkakati wa TANESCO wa kuhakikisha elimu kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia inawafikia wananchi wengi zaidi.

“TANESCO Kinondoni Kaskazini tutaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo watu mashuhuri, ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu faida za kutumia umeme kwa shughuli za kupikia na hivyo kuongeza matumizi ya nishati safi nchini,” amesema Mha. Mathayo.
Amesema kupitia kampeni hizo wananchi wanaendelea kupata elimu inayowawezesha kufanya maamuzi sahihi ya matumizi ya nishati, huku wakinufaika na umeme ambao ni salama, rahisi kutumia, unaookoa muda na rafiki kwa mazingira.
Kwa TANESCO, kampeni hiyo inaendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa wateja na kuongeza matumizi yenye tija ya umeme, sambamba na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali katika kufikisha huduma karibu zaidi na wananchi.
Jitihada hizo pia zinaunga mkono ajenda ya Serikali ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, hatua inayochangia kulinda mazingira, kuboresha afya za wananchi na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.


