Na Mwandishi Wetu
JESHI la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam limewakamata watu 37 kwa tuhuma za makosa ya kimtandao ikiwemo kutoa vitisho na kutumia lugha chafu mtandaoni, hatua ambayo imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama wa kidijitali katika Jiji la Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Aprili 27, 2026, watuhumiwa hao wamekamatwa Aprili 20, 2026 katika eneo la Ubungo kufuatia operesheni maalum iliyotegemea taarifa kutoka kwa wananchi na wadau wa usalama, ambapo baadhi yao wamebainika kuwa wafanyakazi wa kampuni zinazotoa huduma za mikopo kwa njia ya mtandao.
Aidha, baadhi ya Watuhumiwa waliotajwa ni pamoja na Renatus Mujwahuzi maarufu Migeyo Mkazi wa Mbezi Beach, Odilia Oswin maarufu Ngunga Mkazi wa Goba Njia Nne pamoja na Theresia Brastius maarufu Kanu Mkazi wa Mtoni Kijichi huku wengine 34 wakiendelea kushikiliwa na kufanyiwa uchunguzi zaidi.
Pamoja na hayo, Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam wamesema wanaendelea na hatua za kisheria dhidi ya watuhumiwa hao, huku wakisisitiza dhamira yao ya kudhibiti vitendo vya kihalifu mtandaoni vinavyoathiri ustawi wa jamii na usalama wa raia, na kutoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa taarifa za vitendo vya kihalifu ili viweze kufanyiwa kazi kwa haraka na wahusika kufikishwa Mahakamani kwa mujibu wa sheria zilizopo nchini.


