Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imekabidhi hundi ya shilingi 94.1 bilioni kwa ajili ya mikopo ya wanawake, vijana, watu wenye ulemavu, wafanyabiashara wadogo, wakiwemo mamalishe na babalishe, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha kukuza mitaji na kuimarisha shughuli zao za kiuchumi.
Hundi hiyo imekabidhiwa leo Jumanne Aprili 21, 2026 na Rais Samia Suluhu Hassan kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Profesa Riziki Shemdoe, kwa niaba ya kundi hilo.
Katika kongamano hilo, Rais Samia pia ametunukiwa Tuzo ya Malkia wa Nishati Safi iliyotolewa na Umoja wa Mamalishe (Umalita), ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini.


Akizungumza katika kongamano hilo, Rais Samia amesema shughuli za Mama Lishe na Baba Lishe zinapaswa kutambuliwa na kuheshimiwa kutokana na mchango mkubwa wanaoutoa katika maisha ya kila siku ya Watanzania.
“Mtakubaliana nami kwamba shughuli za Mamalishe na Babalishe zinastahili kutambuliwa na kuheshimiwa kwa hadhi inayolingana na mchango wao katika maisha yetu ya kila siku. Yale yaliyosemwa hapa ya kunyanyaswa, ya kusumbuliwa, hayapaswi kufanywa kwa kundi hili,” amesema.
Amesema kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha wafanyabiashara hao wadogo kufanya kazi zao kwa utulivu na usalama, huku akiwataka viongozi wa maeneo mbalimbali kuacha vitendo vya unyanyasaji dhidi yao.


