Na Mwandishi Wetu
Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) imetoa bei mpya za nauli kwa mabasi yanayofanya safari za mikoani, mabasi ya mijini (daladala), teksi mtandao pamoja na pikipiki mtandao.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana Aprili 17, 2026 kupitia Gazeti la Serikali, bei mpya zitaanza kutumika Mei mosi 2026 ikiwa ni baada ya siku 14 tangu kutangazwa rasmi.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa mabasi ya mijini (daladala), viwango vipya vinaonyesha kwamba safari ya hadi kilomita 10 itagharimu Sh 700, ikimaanisha kuwa nauli imeongezeka kulingana na umbali hadi kufikia Sh 1,500 kwa safari ya kilomita 36 hadi 40.
Kabla ya ongezeko hilo nauli zilikuwa zinaanzia Sh 600 kwa umbali usiozidi kilometa 10 ambako kwa sasa imeongezeka hadi Sh 700, pia umbali wa kilometa 34 hadi 40 ilikuwa Sh 1,400 ambako sasa itakuwa Sh 1,500.
Taarifa hiyo imebainisha kuwa wanafunzi wataendelea kulipa Sh 200 kwa safari bila kujali umbali. Huku teksi mtandao, nauli zikipangwa kwa viwango vya chini na juu.
Imesema safari isiyozidi kilomita moja, abiria atalipa kati ya Sh 4,000 hadi Sh 5,000, huku gharama ya kuanzia safari ikiwa kati ya Sh 1,100 na Sh 1,200.
Pia nauli kwa kila kilomita ni kati ya Sh 1,100 hadi Sh 1,300 na kwa dakika ni kati ya Sh 120 hadi Sh 150.
Katika jedwali la nauli za mabasi ya masafa marefu zimepangwa kulingana na daraja la basi na hali ya barabara. Kwa mabasi ya kawaida (ordinary), abiria atalipa Sh 57.93 kwa kilometa moja katika barabara ya lami na Sh 66.62 kwa barabara ya vumbi.
Mabasi ya kati (semi-luxury), nauli kwa kilometa moja kwenye barabara ya lami ni Sh 74.18.


