Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza bei mpya za mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa zilizoanza kutumika rasmi kuanzia leo Aprili Mosi, 2026, ambapo bei za rejareja jijini Dar es Salaam petroli inauzwa kwa Sh. 3,820 kwa lita, dizeli Sh. 3,806 na mafuta ya taa Sh, 3,684 kwa lita.
Maeneo mengine kama Tanga Petroli itapatikana kwa Sh. 3,881, dizeli 3,867 na mafuta ya taa 3,745, Mtwara Petroli ni Sh. 3,912, dizeli itauzwa kwa Sh. 3,898 na mafuta ya taa Sh. 3,777 huku maeneo mengine petroli ikiwa ni zaidi ya Sh. 4000.
Bei zilizotangazwa leo na EWURA, ni tofauti na bei zilizotangazwa Machi 4, 2026, ambapo amaeneo mengi mafuta yaliuzwa ni Sh. 2,864 hadi Sh. 2, 959.
Taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), imeeleza kuwa ongezeko hilo kubwa la bei, limetokana na athari za mzozo wa kivita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.
EWURA imesema, mashambulizi katika visima vya mafuta, maghala na viwanda vya kusafisha mafuta Mashariki ya Kati pamoja na kufungwa kwa Lango la Hormuz, kumeathiri gharama za uagizaji wa mafuta nchini.
Pia hali hiyo imeongeza gharama za usafirishaji wa mafuta kutokana na upungufu wa meli za mizigo pamoja na kuongezeka kwa gharama za bima, jambo ambalo limeathiri moja kwa moja nchi kama Tanzania inayotegemea uagizaji wa mafuta kutoka nje.
Aidha imewataka wauzaji wa mafuta kuzingatia bei elekezi zilizotolewa na kuweka wazi bei hizo katika mabango yanayoonekana kwa urahisi kwa wateja.
Akizungumzia hali ya kupanda kwa mafuta bungeni Dodoma leo, Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaketi ili kuangalia uwezekano wa kuleta unafuu kwa Watanzania.


