Na Tatu Mohamed
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa matanki 15 ya kuhifadhia mafuta itakayofanyika Machi 3, 2026, katika Bandari ya Dar es Salaam.
Akizungumza Machi 2, 2026, Waziri wa Uchukuzi, Makame Mbarawa, amesema hafla hiyo ni sehemu ya mpango mpana wa Serikali wa kupanua na kuboresha bandari hiyo ili kuimarisha nafasi yake kama lango kuu la biashara nchini na katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Prof. Mbarawa ameeleza kuwa ujenzi wa matanki hayo 15 utaongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa taifa katika kuhifadhi mafuta, kuboresha mnyororo wa usambazaji wa nishati, na kuchochea ukuaji wa biashara za ndani na za kimataifa.
Amesisitiza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika eneo la ukanda.

“Mradi huu unaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha miradi ya kimkakati inayochochea maendeleo ya nchi,” amesema Prof. Mbarawa.

Maboresho hayo ni sehemu ya uwekezaji unaoendelea katika Bandari ya Dar es Salaam, yakilenga kuongeza ufanisi wa huduma, kuvutia wawekezaji zaidi, na kuimarisha ushindani wa bandari hiyo katika soko la kimataifa.


