Na Mwandishi Wetu
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali, Hamza Johari amesisitiza juu ya umuhimu wa kutambua mabadiliko na mageuzi makubwa ya kiteknolojia kunakopelekea ongezeko la matumizi ya Akili Bandia (AI), ndege zisizo na rubani, mifumo ya kidijitali na vitisho vya usalama mtandao.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameyasema hayo tarehe 25 Februari, 2026 wakati alipokuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Warsha ya siku 3 iliyoandaliwa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) na Shirika la Kimataifa la Usimamizi wa Anga Duniani (ICAO) kuhusu Sheria na Kanuni za Usafiri wa Anga inayofanyika kuanzia tarehe 25 hadi 27 Februari, 2026 Jijini, Dar es Salaam.

“Ingawa teknolojia hizi zinafungua fursa kubwa za ubunifu na ufanisi, pia zinaibua maswali magumu ya kisheria na kimaadili, ni muhimu kwa nchi kutafakari upya namna ya kutunga, kusimamia na kutekeleza sheria za anga.” Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Ameeleza kuwa usafiri wa anga una mchango mkubwa katika kuunganisha watu, masoko na tamaduni, kuchochea ukuaji wa uchumi, biashara na utalii. Huku akisisitiza kuwa manufaa hayo yanategemea mfumo thabiti na ulioratibiwa wa sheria za kimataifa za anga.
Aidha, Johari amewataka washriki wa warsha hiyo kuangalia kwa kina maudhui ya sheria za anga na kuhimizana kuhakikisha kuwa nchi ambazo bado hazijaridhia mikataba ya anga na kuingiza katika sheria zao ziweze kuridhia na kuingia katika Mikataba hiyo.

“Muutumie mkutano huu katika kujadili kwa kina juu ya maudhui mbalimbali ya sheria za anga, pia kuhimizana kuhakikisha kuwa nchi ambazo hazijaridhia mikataba hii ya kimataifa zifanye hivyo na kuingiza katika sheria zao.” Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Vilevile, Mwanasheria Mkuu wa Serikali amezungumzia umuhimu na faida za nchi kuridhia na kuingia katika mikataba mbalimbali ya Kimataifa ya Anga, ambapo ameisisitiza Mamlaka ya Usafiri wa Anga kuhakikisha mikataba ya anga ambayo nchi haijaingia iweze kiridhiwa na kuwekwa katika Sheria ili kurahisisha shughuli za usafiri wa anga.

“Watalaamu na Wanasheria mlioko hapa mjadiliane kwa kina na kubadilisha uzoefu juu ya namna gani mnaweza kuhakikisha kwamba changamoto zote zilizoko katika sheria za anga zinatatuliwa.” Amesema Johari.
Awali, akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga, Salim Msangi amesema kuwa Warsha hiyo ni fursa kwa wataalamu na Wanasheria katika kuielewa Mikataba mbalimbali ya Anga, kwani itasaidia sheria mbalimbali za anga ziweze kutekelezeka na kufanya Usafiri wa Anga uweze kukua.

“Kikao hiki tunatumia kama fursa ya kuweza kuielewa mikataba mbalimbali ya Kimataifa ya Anga kwakuwa kupitia mikataba hii tutaweza kuboresha na kukuza usafiri wa anga nchini.” Amesema Msangi.

Warsha ya kupitia Sheria na Kanuni za Usafiri wa Anga iliyoandaliwa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) na Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga Duniani (ICAO) inawahusisha washiriki takribani 150 kutoka mataifa mbalimbali Duniani na itafanyika kwa siku 3 kuanzia tarehe 25 hadi 27 Februari, 2026 Jijini Dar es Salaam.


