Na Mwandishi Wetu
Rais Samia Suluhu Hassan, leo Februari 24, 2026, amezindua jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa lililojengwa katika eneo la Kikombo, jijini Dodoma, huku akilitaka Jeshi la Tanzania kuhakikisha miundombinu hiyo inatumika kikamilifu kuimarisha ulinzi na usalama wa taifa.
Ujenzi wa jengo hilo ulianza wakati wa Serikali ya Awamu ya Tano, ambapo jiwe la msingi liliwekwa Novemba 25, 2019, na aliyekuwa Rais wa awamu hiyo, Hayati John Magufuli.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Rais Samia amesema kuwa jengo jipya la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa ni alama ya ukomavu wa taifa na uthibitisho wa uwezo wa Watanzania kupanga, kuamua na kutekeleza miradi mikubwa kwa kutumia rasilimali na wataalamu wa ndani.

Amesema uwekezaji huo unaimarisha uhuru wa maamuzi ya taifa na kulipa heshima katika masuala ya ulinzi barani Afrika, akibainisha kuwa Tanzania sasa ni miongoni mwa nchi zinazotoa kipaumbele cha juu kwa shughuli za ulinzi.
Amesisitiza kuwa makao makuu hayo yanapaswa kuwa kituo cha fikra, uchambuzi wa kitaalamu na uratibu wa kisayansi wa mikakati ya ulinzi inayoendana na mabadiliko ya wakati.
Rais Samia ameeleza kuwa katika mazingira ya sasa ya usalama wa dunia, ulinzi hauhusiani na silaha pekee, bali unategemea pia upatikanaji na uchambuzi wa taarifa, matumizi ya teknolojia za kisasa, mifumo madhubuti ya mawasiliano pamoja na ubobezi wa hali ya juu wa kitaalamu.

Amebainisha kuwa baada ya kulitembelea jengo hilo, ameridhishwa na hatua zilizofikiwa katika kuzingatia matumizi ya teknolojia na mifumo ya kisasa, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza nguvu katika awamu zijazo za ujenzi.
Aidha ameahidi kuhakikisha kuwa awamu zilizobaki za mradi huo zinakamilishwa kwa wakati ili kuendelea kuimarisha uwezo wa taifa katika kulinda mipaka, maslahi na usalama wa nchi
Kwa upande wake Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Jacob Mkunda, amesema gharama zilizotumika kukamilisha ujenzi wa jengo hilo na miundombinu iliyopo ni Sh. 212 bilioni ambapo fedha zote zimetolewa na Serikali.
“Makao Makuu haya ya kudumu ya ulinzi wa taifa ni ya kwanza kabisa kihistoria katika jeshi letu. Kama wote mnavyojua, kabla ya makao makuu haya, jeshi lilikuwa na makao makuu yake Upanga, Dar es Salaam, tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964,” amesema Jenerali Mkunda.


