Na Mwandishi Wetu
ALIYEKUWA Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Polycarp Kardinali Pengo amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 81.
Taarifa rasmi ya kifo chake imetolewa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Yude Ruwai’chi, usiku wa kuamkia leo Ijumaa, Februari 20, 2026.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Kardinali Pengo alifariki dunia majira ya saa 4:00 usiku wa Alhamisi, Februari 19, 2026, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), jijini Dar es Salaam.

Askofu Mkuu Ruwai’chi amesema kuwa Kanisa linaendelea kuungana na waumini pamoja na Watanzania wote katika kipindi hiki cha maombolezo, huku akiahidi kuwa ratiba na taratibu za mazishi zitatangazwa baadaye.
Kardinali Pengo alizaliwa Agosti 05, 1944 na alitumikia Kanisa Katoliki kwa zaidi ya nusu karne katika nafasi mbalimbali za uongozi.
Aliwahi kuwa Askofu wa Jimbo la Nachingwea kabla ya kuteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Dar es Salaam mwaka 1992.
Mwaka 1998, aliteuliwa kuwa Kardinali na Hayati Papa Yohane Paulo wa Pili, hatua iliyomfanya kuwa miongoni mwa viongozi wa juu wa Kanisa Katoliki duniani.
Katika kipindi cha uongozi wake, Kardinali Pengo alijulikana kwa misimamo yake katika masuala ya kijamii, maadili na maendeleo ya taifa, akisisitiza umoja, amani na mshikamano wa Watanzania.
Alistaafu rasmi mwaka 2019 lakini aliendelea kutoa ushauri na mafundisho ya kiroho kwa jamii.
Kifo chake ni pigo kubwa kwa Kanisa Katoliki na taifa kwa ujumla, kikiacha pengo kubwa katika uongozi wa kiroho nchini.


