Na Tatu Mohamed
MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa mwelekeo wa mvua za msimu wa Masika kwa kipindi cha Machi hadi Mei 2026, ikitabiri uwepo wa mvua za wastani hadi juu ya wastani katika maeneo mengi ya pwani ya kaskazini pamoja na baadhi ya maeneo ya magharibi mwa Ukanda wa Ziwa Victoria.
Akitoa mwelekeo wa mvua hizo leo Februari 05, 2026 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dkt. Ladislaus Chang’a amesema mvua zinatarajiwa kuanza kunyesha katika wiki ya nne ya Februari na wiki ya kwanza ya Machi 2026 katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria.
Amefafanua kuwa maeneo ya Pwani ya Kaskazini yanatarajiwa kupata mvua kuanzia wiki ya kwanza na ya pili ya Machi, huku maeneo ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki yakitarajiwa kuanza kupata mvua kuanzia wiki ya pili na ya tatu ya Machi 2026.

“Mvua za Masika zinatarajiwa kuisha kati ya wiki ya nne ya mwezi Mei na wiki ya kwanza ya mwezi Juni 2026 katika maeneo mengi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka,” amesema Dkt. Chang’a.
Ameongeza kuwa kiwango kikubwa cha mvua kinatarajiwa kuanza kushuhudiwa mwezi Aprili 2026, akieleza kuwa mwelekeo huo umezingatia zaidi kipindi cha miezi mitatu ya Masika pamoja na hali ya mvua katika maeneo makubwa ya nchi.
“Mwelekeo wa mvua uliotolewa umezingatia zaidi kipindi cha mvua za Masika na hali ya mvua katika maeneo makubwa, huku mabadiliko ya muda mfupi yakizingatiwa kupitia utabiri wa kila siku na wa kila mwezi,” amefafanua.

Dkt. Chang’a ametoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali kuendelea kufuatilia taarifa rasmi za hali ya hewa zinazotolewa na TMA.
“Tunawashauri watumiaji wa taarifa za hali ya hewa kufuatilia utabiri wa saa 24, siku 10, utabiri wa mwezi pamoja na tahadhari mbalimbali zinazotolewa na TMA,” alisisitiza.
Ameeleza kuwa mvua za Masika ni mahususi kwa maeneo ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, pwani ya kaskazini, Ukanda wa Ziwa Viktoria pamoja na kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma. Kwa mujibu wa TMA, katika baadhi ya maeneo ya magharibi mwa Ukanda wa Ziwa Victoria ikiwemo mikoa ya Kagera na Geita pamoja na kaskazini mwa Kigoma, mvua zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani.

Hata hivyo, katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu, mvua zinatarajiwa kuwa za wastani hadi chini ya wastani, zikianza kati ya wiki ya nne ya Februari na wiki ya kwanza ya Machi na kuisha wiki ya tatu na ya nne ya Mei 2026.
Aidha, amesema TMA inaendelea kutoa ushauri kwa sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo kilimo, mifugo, uvuvi, usafiri, ujenzi, nishati, maji, madini pamoja na mamlaka za serikali za mitaa ili zipange shughuli zao kwa kuzingatia taarifa za hali ya hewa.


