Na Winfrida Mtoi
LIGI Kuu Tanzania Bara imeendelea leo Novemba 7, 2025 kwa michezo miwili kupigwa ambapo Yanga na Azam zimefanikiwa kuondoka na alama tatu kila mmoja, huku Mnyama Simba akiambulia kichapo.
Yanga imeibuka na ushindi wa bao 1-0 mbele ya Coastal Union kwenye dimba la Jamhuri Dodoma, wakati Azam imeipiga Simba mabao 2-0 Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam.
Bao pekee la Yanga lilifungwa na Prince Dube dakika ya 88, huku mabao ya Azama yakifungwa na Jephte Kitambala dakika 81 na Idd Seleman ‘Nado’ dakika ya 89.


Matokeo ya Simba yamewafanya mashabiki wake waondoke uwanjani kwa hasira huku wakiwatupia lawama viongozi wa klabu hiyo.
Kocha wa Simba Selemani Matola ametaja kile kilichowaangusha kuwa ni kupoteza umakini kwa wachezaji wake dakika za jioni.
Kwa upande wake kocha wa Azam FC, Florent Ibenge amesema mchezo ulikuwa mgumu lakini mabadiliko aliyofanya kipindi cha pili yamempa matokeo mazuri.


