Mwandishi Wetu
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, leo Juni 16, 2025, amezindua kiwanda cha kutengeneza mabomba ya maji na uchakataji wa pamba cha MOLI Oil Mills Co. Ltd kilichopo Bariadi, Mkoa wa Simiyu.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza ajira lakini pia pamba inayozalishwa ndani ya nchi kutumika hapa nchini kuzalisha bidhaa nyingine badala ya kuisafirisha nje ya nchi kama ambavyo inavyofanyika sasa.



“Tunajua kwamba Simiyu zao kubwa la kiuchumi ni pamba ukiacha mengine na nimshukuru mwekezaji hapa wa ndani amewaza kuongeza thamani angalau kwa hatua ya kwanza, lakini hatua ya pili sasa tutanunua kwake kuweka kwenye kiwanda ambacho tayari tumeanza kukijenga cha kutengeneza nyuzi za pamba.

“ Tunataka kusitisha kupeleka pamba yetu kama ilivyo kwenye marobota kwa wenzetu wakatengeneze nguo na watu wao wapate kazi, tunataka pamba yetu tuitengeneze hapa hapa ili watu wetu wa Simiyu waweze kupata ajira ndani ya mkoa huu,” amesema Rais Samia.