Na Mwandishi Wetu
USAFIRI umeanza kurejea katika barabara kuu kutoka Dar es Salaam kwenda Lindi baada ya wataalamu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kufanya kazi usiku na mchana kurekebisha eneo la Somanga Matandu lililoharibiwa na mvua na kufanya njia isipitike.
Daraja la Somanga lilikatika Aprili 06, 2025 huku lile la Mto Matandu likikatika Aprili 07, 2025 na kusababisha adha kwa abiria wanaotumia Barabara hiyo.
Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega ambaye ameweka kambi katika eneo hilo tangu jana, amewaambia waandishi wa habari kuwa magari madogo 230, mabasi 10 na baadhi ya malori 30 yaliyobeba bidhaa mbalimbali yakiwemo mawe makubwa yamefanikiwa kupita katika eneo la Somanga Mtama na Matandu leo kati ya saa 11:30 alfajiri hadi saa 12:00 asubuhi.

Ulega ameyasema hayo leo Aprili 8, 2025 wakati akitoa taarifa ya awali akiwa mkoani Lindi wakati akiendelea kusimamia zoezi la urejeshaji wa maeneo yaliyokatika katika barabara kuu ya Dar es Salaam – Lindi linaoofanywa na wataalamu wa Wizara ya Ujenzi na TANROADS kwa kushirikiana na mkandarasi.