Na Mwandishi Wetu
JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linawashikilia raia wanne wa China kwa tuhuma za kuhusika na tukio la utekaji wa wafanyabiashara wenzao wawili, Weiyi Chen (64) na Liang Xiolo (44).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro tukio hilo lilitokea Mei 14, 2026 saa 4:30 usiku katika majengo ya PSSSF, Mtaa wa Mission, Ilala.
Watuhumiwa waliokamatwa ni Deng Anqing (49), Fan Zhong (49), Zhang Jianjun (52) na Deng Qiang (40), ambapo walikutwa na simu za wahanga pamoja na vielelezo vingine vinavyohusishwa na tukio hilo.
Inadaiwa kuwa wafanyabiashara hao walivamiwa na kundi la watu saba na kutekwa kwa nguvu kisha kupelekwa kusikojulikana huku watuhumiwa wakidaiwa kutaka fidia ya dola za Marekani milioni 20 kutoka kwa ndugu ili kuwaachia huru.
Taarifa hiyo imesema Polisi waliweza kufuatilia magari yaliyotumika katika tukio hilo ikiwemo Toyota Alphard yenye namba bandia T.305 DRP pamoja na Toyota Harrier yenye namba T.188 DHT.
“Baada ya msako mkali uliofanyika Mei 16, 2026 Jeshi la Polisi liliwafuatilia na kuwabaini wahanga hao katika eneo la Mbezi, Kinondoni wakiwa wamejeruhiwa sehemu mbalimbali za miili yao ambapo walikimbizwa hospitalini kwa matibabu huku Weiyi Chen akiendelea kupatiwa huduma kutokana na hali yake kutokuwa nzuri,”


