Na Mwandishi Wetu, Dodoma
TAASISI ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) imewataka wakulima nchini kuhakikisha wananunua mbegu zenye lebo ya uthibitisho ya taasisi hiyo, ikionya kuwa mbegu zisizo na lebo hiyo zinaweza kuwa bandia na kusababisha hasara katika uzalishaji.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Nyasebwa E. Chimagu, alisema lebo ya TOSCI ndiyo uthibitisho kuwa mbegu imekaguliwa na kuthibitishwa ubora wake kabla ya kuingia sokoni.
Alisema wakulima wanapaswa kuhakikisha mbegu wanazonunua zimefungashwa katika vifungashio rasmi vyenye lebo ya TOSCI na kuhakiki uhalali wa lebo hiyo kwa kutumia simu za mkononi ili kujiridhisha kuwa mbegu hizo ni halisi.
“Hatua hiyo itawasaidia wakulima kuepuka kununua mbegu bandia ambazo zinaweza kusababisha hasara na kupunguza uzalishaji,” alisema Chimagu.

Alibainisha kuwa matumizi ya mbegu bora ndiyo msingi wa kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao na yana mchango muhimu katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Kwa mujibu wa Chimagu, matumizi ya mbegu zilizothibitishwa pamoja na kuzingatia kanuni bora za kilimo yanaweza kumwezesha mkulima kuvuna kati ya tani tano hadi 10 kwa hekta, kutegemeana na aina ya zao na mazingira ya uzalishaji.
Aidha, alisema TOSCI inaendelea kutumia Maonesho ya Nanenane kutoa elimu kwa wakulima, wazalishaji na wafanyabiashara wa mbegu kuhusu umuhimu wa kutumia mbegu bora pamoja na kufuata taratibu za uzalishaji, usafirishaji na biashara ya mbegu.
Aliwahimiza wakulima kutumia fursa ya maonesho hayo kutembelea banda la TOSCI ili kupata elimu kuhusu mbegu zilizothibitishwa na teknolojia mbalimbali za kilimo zitakazowawezesha kuongeza tija katika msimu wa kilimo wa mwaka 2026/2027.


