Na Mwandishi Wetu
MAHAKAMA ya Rufani Tanzania leo 15 Aprili 2026, imekiondolea kifungo cha kutofanya shughuli za kisiasa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa kuondoa zuio hilo lililowekwa na Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dar es Salaam.
Katika hukumu hiyo imetolewa jijini Dodoma na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, Jaji Augustine Mwarija, Jaji Issa Maige na Jaji Abraham Mwampashi.
Uamuzi huo umetokana na mashauri ya mapitio ya Mahakama yaliyofunguliwa na Mahakama yenyewe kutokana na kesi ya msingi ya madai ya mgawanyo usio sawa wa rasilimali za chama hicho baina ya Bara na Zanzibar.
Kesi hiyo imefunguliwa Mahakama Kuu Dar es Salaam na Makamu Mwenyekiti mstaafu wa Chadema, Said Issa Mohamed, pamoja na wajumbe wawili wa Bodi ya Wadhamini wa Chadema kutoka Zanzibar, Ahmed Rashid Khamis na Maulida Anna Komu.
Hata hivyo, Mahakama ya Rufani, baada ya kuitisha na kusikiliza mashauri ya mapitio ya mwenendo na uamuzi mdogo wa Mahakama Kuu kuhusiana na kesi ya msingi na mashauri madogo yaliyotokana na kesi hiyo, likiwemo la zuio hilo la kufanya siasa, imetengua uamuzi huo wa zuio.


