Na Mwandishi Wetu
RIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), imebaini kuwa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) imeendelea kupata hasara baada ya ripoti mpya kwa mwaka wa fedha wa 2024/2025 kuonyesha kuwa kampuni hiyo imepata hasara ya shilingi bilioni 191.19.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, hasara hiyo ni ongezeko la asilimia 108 ikilinganishwa na mwaka uliopita, jambo linalofanya jumla ya hasara tangu kuanzishwa kwa shirika hilo kufikia shilingi bilioni 748.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere amebainisha hayo leo Machi 30, 2026 wakati akiwasilisha ripoti yake ya ukaguzi wa fedha kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Ameeleza kuwa licha ya ATCL kupokea ruzuku kutoka serikalini kwa ajili ya kulipa mishahara na gharama za uendeshaji, shirika hilo limekumbwa na changamoto kubwa ya gharama za uendeshaji kuzidi ukuaji wa mapato, gharama za uendeshaji kwa sh bilioni 134 na kufikia sh bilioni 675.
“Sababu zinazochangia hasara hiyo kuwa ni changamoto za kiutendaji na safari za ndege, ufanisi wa safari za ndege kuwa chini ya matarajio ambapo katika njia 87 za safari, wastani wa ujazo wa abiria (load factor) ulikuwa ni asilimia 55 pekee,” amesema Kichere.
Aidha, kumebainisha kuwa matumizi ya sio bora ya ndege ya mizigo aina ya Boeing 767-300F, ikitumika kinyume na matumizi yaliyokusudiwa, ambapo asilimia 94 ya safari zake zilikuwa za masafa mafupi na kati badala ya safari ndefu ambazo zingeweza kuzalisha mapato makubwa zaidi.
Amefafanua kuwa hali imekuwa mbaya zaidi baada ya ndege hiyo kusimamishwa kazi, huku ikiendelea kugharimu shirika takriban sh bilioni 3.54 kwa ajili ya ukodishaji na bima bila kuzalisha mapato yoyote.
Pia uwepo wa udhaifu wa mifumo ya udhibiti wa ndani,ripoti hiyo ikibaini kuwepo kwa malipo ya sh bilioni 20.61 yaliyofanywa kwa mawakala bila kuwepo kwa uthibitisho wa kuwafikia abiria.


