Na Mwandishi Wetu
WAKATI Yanga ikitarajiwa kushuka dimbani kesho Machi 18, 2026 kuikabili TRA United katika Ligi Kuu Tanzania, timu hiyo itawakosa wachezaji wake muhimu wanaokabiliwa na majeraha akiwamo mshambuliaji Laurindo Dilson ‘Depu’.
Akizungumza na waandishi wa habari kuelekea mchezo huo utakaopigwa kesho saa 10:00 alasiri, katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha, Kocha Mkuu wa Yanga Pedro Goncalves amesema wamekuwa na ratiba ngumu ya michezo mfululizo ukizingatia wametoka kucheza mechi ngumu siku chache zilizopita tofauti na wapinzani wao.
Amesema wanakwenda kukabiliana na timu ambayo imepata muda wa kutosha wa mapumziko na maandalizi lakini wamejipanga kuchukua pointi tatu.
“Pia tumekubwa na idadi kubwa ya majeruhi. Lakini hali hiyo inatoa fursa kwa wachezaji wengine wenye hali nzuri,” amesema.
Uongozi wa Klabu ya Yanga umetoa taarifa ya kuthibitisha kuwa wachezaji wake wanne wakiwemo Chadrack Boka, Edmund John pamoja na Ibrahim Abdullah ‘Bacca’ wamepata majeraha na wanatarajiwa kuwa nje ya uwanja kwa wiki kadhaa.
Wachezaji wengine ni Chadrack Boka ambaye amepata jeraha la enka ya mguu wa kushoto na atakuwa nje ya uwanja kwa kipindi cha wiki mbili, na Edmund John ambaye amepata jeraha la bega na atakuwa nje ya uwanja kwa kipindi cha wiki mbili.


